ASKARI WA USALAMA BARABARANI KIGOMA, HII INAWAHUSU

Mkuu wa Kikosi cha Usalama barabarani nchini, Kamanda Fortunatus Musilimu.
Na Mtapa Wilson

Mazoea hujenga kawaida.  Hivi ndivyo unavyoweza kusema ukisafiri katika barabara ya kutoka Kigoma mjini kwenda Manyovu, mpakani mwa Tanzania na Burundi.
 
Utaona gari ndogo aina ya Noah na taksi nyingi aina ya ‘Toyota Pro box’ maarufu kama ‘mchomoko’ zikibeba abiria na mizigo huku zikisafiri umbali wa kilomita zaidi ya 60.

Pata picha gari yenye uwezo wa kubeba abiria watano inabeba abiria 10 mpaka 12.  Wakati mwingine gari inayobeba abiria nane inabeba abiria 15 mpaka 20 huku ikichanganya na mizigo ya mikungu ya ndizi na nanasi.

Tatizo kubwa ni abiria wengi kutokufunga mikanda ya usalama wanapokuwa ndani ya usafiri huu mashuhuri huko Manyovu kutokana na kujazana wengi ndani ya gari mithili ya nyanya kwenye tenga.

Katika uchunguzi wa mwandishi aliyesafiri kwa usafiri wa ‘mchomoko’ mara kadhaa barabara ya Manyovu alishuhudia ‘mchomoko’ namba T428 DEE wenye uwezo wa kubeba abiria 5 ukiwa umebeba abiria 10, ambao hawakufunga mkanda, wakiwa wamejezana pamoja na mizigo ya matunda mbalimbali.

Aidha mwandishi aliona ‘mchomoko’ namba T479 ALR umejaza abiria bila kufunga mikanda huku wengine wakikaa nyuma ya buti pamoja na mafurushi ya nanasi na mikungu ya ndizi.

Imeelezwa kuwa uchanganyaji wa abiria na mizigo katika magari ya abiria imekuwa ni hali ya kawaida kwasababu wakazi wengi wa Manyovu, ambao ni wafanyabiashara hutegemea zaidi usafiri wa ‘mchomoko’ kwajili ya kusafirishia bidhaa zao kwenda mnadani kama vile Kalinzi na Kigoma mjini kwa madai ya kuwa ni usafiri nafuu ukilinganisha na magari rasmi yanayobeba mzigo.

Sheria ya usalama barabarani ya mwaka 1973 kifungu cha 39 inakataza dereva wa chombo cha moto kubeba mzigo wenye uzito mkubwa ukilinganisha na uwezo wa gari.  Pia inamkataza dereva kubeba idadi kubwa ya abiria ukilinganisha na uwezo wa gari husika.

Aidha sheria hiyo inaelekeza kwa dereva atakayekiuka kulipa faini isiyopungua kati ya shilingi 20,000 na 50,000 au kifungo kisichopungua miaka mitatu ama adhabu zote mbili kwa mpigo.

Kuna wakati mwandishi alipanda gari aina ya Toyota Noah namba T663 DDF ambapo dereva alibeba abiria takribani 20 kwa kuwabananisha bila kufunga mikanda.
Dereva wa gari hilo, Rashid Mussa (30), alisema wanalazimika kubeba abiria wengi kwasababu ya kutengeneza faida kubwa.

Alisema kubeba abiria kulingana na uwezo wa gari unatia hasara kwakuwa wanasafiri umbali mrefu na nauli inayolipwa na abiria ni kiduchu mno.

“Kama unavyoona gari ni nyingi.  Hapa tulipo tunapakia kwa foleni. Ili upate faida ni lazima ubebe abiria wengi zaidi.  Vinginevyo utakuwa unafanya kazi bure,” alisema.

Deogratius Ramadhan ni mmiliki na dereva wa ‘mchomoko’ namba T219 ATS alisema mbali na faida inayopatikana kwa kujaza abiria lakini ukweli ni kwamba, abiria walio wengi wanakabiliwa na umasikini mkubwa, hivyo huomba msaada wa nauli pungufu, hali inayowalazimu kuwabeba wengi kwa kufidia gharama hiyo.

“Mie Manyovu ndio nimezaliwa na kukulia. Unakuta nipo kazini anakuja jirani kabisa anajua nauli 5,000 lakini yeye anataka umbebe kwa 2,000 au 3,000.  Siwezi kumuacha kwa ujamaa tulionao.  Hapo sasa inanibidi nibebe abiria zaidi ili kufidia wanaolipa kidogo,” alisema.

Pamoja na changamoto ya abiria na mizigo kujazwa kupita kiasi katika ‘michomoko’ hiyo, hakuna sehemu hata moja ambayo mwandishi alishuhudia ukaguzi wa askari ukifanyika na hatua zikichukuliwa.

Barabara ya Manyovu ina vizuizi takribani vinne ambavyo vinakaliwa na askari.  Lakini mwandishi aliweza kupita akiwa ndani ya ‘michomoko’ iliyojaza abiria wengi na mizigo kupita uwezo wake lakini iliruhusiwa kupita bila bughuza yoyote.

Akiwa ndani ya usafiri huo, mwandishi alipita katika vizuizi vya askari maeneo ya Mwandiga kwa Zitto, Kalinzi, Kasagamba na Kiremba ingawa abiria wote walikuwa hawakufunga mikanda.

kwa mujibu wa Sumatra magari madogo ya abiria kama vile Noah yanaruhusiwa kusafiri umbali usiozidi kilomita 50, lakini hali ni tofauti katika eneo la Manyovu, ambapo  Noah na taksi ‘mchomoko’ zinasafiri umbali zaidi ya kilomita 60 huku abiria wake wakiwa hawajafunga mkanda.

Chiku Shaban (37) ni abiria mkazi wa Manyovu mpakani alisema wapo abiria wanaofahamu umuhimu wa kufunga mikanda ndani ya gari lakini wanashindwa kutokana na kujazana kwa abiria na mizigo ndani ya gari kupita kiasi.

“Unaweza kupanda gari lenye uwezo wa kubeba abiria wanne na dereva wa tano.  Lakini unakuta mnajazwa mpaka 12.  Sasa hapo abiria wote mtafungaje hiyo mikanda?” aliuliza.

Barabara ya Manyovu ina Noah saba na ‘michomoko’ zaidi ya 120, ambayo hubeba abiria na mwandishi alishuhudia mara zote alizopanda usafiri huo, abiria wakiwa hawajafunga mikanda.

Katika uchunguzi wake, Septemba 20, mwaka huu 2017, mwandishi alipata ajali kwenye mchomoko namba T137 DEX katika barabara ya Manyovu akitokea Kigoma mjini kuelekea mpakani katika eneo la Kiremba baada ya taili ya mbele kushoto kupasuka.

Gari iliyumba mara kadhaa njia nzima huku abiria (akiwemo mwandishi) waliokuwa ndani ya gari hilo wakigongana kwa mtikisiko mkubwa kutokana na kutokufunga mikanda ya usalama.

Rhoda Nashon (60) ni mmoja wa abiria mkazi wa Munanila aliyenusurika katika ajali hiyo alisema imekuwa ni kawaida kwa madereva kujaza abiria wengi, hali inayofanya wanashindwa mpaka kufunga mkanda na kujiweka katika hatari pale ajali inapotokea.
“Huku kwetu hata kama gari imejaa lakini bado dereva anapakia.  Hata abiria wenyewe wanaona gari limejaa bado wanaingia,” alisema.

Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, ambaye ni Mwenyekiti wa kamati ya usalama barabarani, Brigedia Jenerali Emmanuel Maganga, alikiri kuwepo kwa tatizo hilo na kudai kuwa wanadhibiti hali hiyo ingawa madereva na abiria wameendelea kufanya hivyo kwa mazoea.

“Tumewahi kulijadili hilo na kuchukua hatua za kuzuia lakini ikaonekana wananchi wameshazoea huo usafiri.  Kwa sasa tumelifumbia macho kidogo wakati tukiendelea na kuandaa mkakati wa kuondoa kabisa tatizo hilo,” alisema.

Afisa leseni na udhibiti usafiri wa barabarani kutoka Mamlaka ya Usafiri wa Majini na Nchi kavu (Sumatra) Mkoa wa Kigoma, Amaniel Sekulu, naye alikiri kupokea taarifa hizo lakini akasema ‘michomoko’ imesajiliwa na Manispaa ya Kigoma Ujiji kama taksi kwa ajili ya huduma za mjini tu lakini inakiuka sheria kwa kusafirisha abiria.

“Mabasi yote yanakaguliwa asubuhi kabla hayajaondoka stendi.  Tunakagua masuala mbalimbali ikiwemo idadi ya abiria na mikanda. Tukimbaini dereva kakiuka sheria tunampiga faini.  Lakini hiyo ‘michomoko’ iko chini ya manispaa, na na huko ndiko wanapata leseni,” anasema.

Mwanasheria wa Manispaa ya Kigoma Ujiji, Emmanuel Mkwe alikana‘michomoko’ hiyo kuwa chini ya manispaa yake kwakuwa walishawafukuza zamani na kuhamia halmashuri ya wilaya ya Kigoma Vijijini, baada ya kushindwa kufuata utaratibu ikiwemo kupaki katika kituo kimoja kwa ajili ya kukodiwa, na siyo kubeba abiria kama inavyofanya sasa.

Afisa biashara wa halmashauri ya Kigoma Vijijini, Boniphace Buberwa alikiri usafiri huo kuhamia katika halmashauri yake tangu mwaka 2014, lakini akasema hawakutoa leseni kutokana na kukosekana kwa sheria ndogo, ambapo walianza kwanza mchakato wa kutunga sheria hizo na zitakapokamilika ndio wataanza kutoa leseni.

“Sasa tupo katika mchakato wa kupitisha mapendekezo ya sheria.  Hao unaowaona sasa wanafanya kazi bubu kwakuwa hawana utaratibu ndio maana wanabeba abiria hovyo,” alisema.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kigoma, Ferdinand Mtui, alisema jeshi limekuwa likifanya ukaguzi wa magari yote katika vizuizi mbalimbali ingawa kuna baadhi ya askari siyo waadilifu ambao huruhusu ‘michomoko’ hiyo kuendelea na safari ijapokuwa imevunja sheria ikiwemo kubeba abiria wengi pasina kufunga mkanda.

“Ni kweli kuna uhuma za rushwa zinazoelekezwa kwa askari wetu.  Tunazipokea.  Lakini wajue kabisa kuna mbinu zetu tutakazozitumia kuwabaini na kuwachukulia hatua zaidi,” alisema.

Pamoja na maelezo hayo, Kamanda Mtui, hakuweza kumweleza mwandishi ni idadi ya askari wangapi ambao wamebainika si waadilifu na hatua zilizochukuliwa dhidi yao ili kuongeza ufanisi wa askari wengine wanaosimamia usalama barabarani ikiwemo abiria kufunga mkanda.

Kutokana na changamoto ya ‘michomoko’ inaripotiwa kuwa mwaka 2016 kulitokea ajali 10 za ‘michomoko’ na kusababisha vifo vya watu saba na kujeruhi mtu mmoja.

Hiyo inaonyesha madhara ya usafiri wa ‘mchomoko’ kwa kusababisha idadi kubwa ya vifo mkoani Kigoma ukilinganisha na wilaya ya Kinondoni ambapo kulitokea ajali za taksi 54 bila kusababisha kifo isipokuwa zilijeruhi watu 18.

Kwa mujibu wa shirika la Afya Duniani (W.H.O), kufunga mkanda kwa abiria wa kiti cha mbele husaidia kwa asilimia 50 uwezekano wa kupata majeraha makubwa pale ajali inapotokea na humsaidia abiria aliyekaa kiti cha nyuma kwa asilimia 75.

Sheria ya usalama barabarani nchini inamtaka dereva na abiria wote kufunga mkanda katika magari ya abiria kama vile mabasi, lakini pia inamtaka dereva na abiria wa kiti cha mbele peke yake kufunga mkanda katika magari madogo binafsi.

Hivyo basi, kuna haja ya kufanya marekebisho katika sheria yetu ili kulazimisha watu wote kufunga mkanda kwa ajili ya kupunguza madhara ya ajali katika gari ndogo kama vile Noah na ‘michomoko’ ambayo maeneo mengi yaliyoko pembezoni mwa mjini inafanya kazi ya kubeba abiria.

Hii inawezekana kwakuwa kuna nchi barani Afrika kama vile Afrika Kusini, Botswana, Namibia, Zambia na hata Malawi, ambazo zina sheria inayolazimisha abiria aliyekaa kiti cha mbele, nyuma pamoja na dereva kufunga mkanda wanapokuwa wamepanda gari.
ASKARI WA USALAMA BARABARANI KIGOMA, HII INAWAHUSU ASKARI WA USALAMA BARABARANI KIGOMA, HII INAWAHUSU Reviewed by Unknown on 15:15 Rating: 5

No comments:

Theme images by merrymoonmary. Powered by Blogger.