UCHUNGUZI: MADEREVA WA BODABODA MWANZA WENGI NI WALEVI


Na Mtapa Wilson, Mwanza

Wakati ripoti ya Shirika la Afya Duniani (W.H.O) ikisema kuwa takribani watu milioni 1.2 wanapoteza maisha kila mwaka kutokana na ajali za barabarani, ambazo kimsingi husababishwa na sababu mbalimbali ikiwemo tabia ya unywaji wa vileo na uendeshaji miongoni mwa madereva.

Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa taarifa hii katika jiji la Mwanza, katika kipindi cha siku 14 yaaani kuanzia Julai 8 mpaka 22, mwaka huu, unaonyesha kuwa tabia ya unywaji wa vilevi na uendeshaji imeendelea kuwa tatizo miongoni mwa madereva wengi wa bodaboda.

Mwandishi alijaribu kutembelea vituo mbalimbali takribani kumi vya waendesha bodaboda vilivyopo katika ya jiji hilo na kufanya uchunguzi ambapo alibaini kuwa katika kila kituo kimoja kuna waendesha bodaboda wawili, watatu, wanne mpaka watano wenye tabia ya kunywa vileo na kuendesha bodaboda.

Aidha uchunguzi unaonyesha kuwa madereva wa bodaboda wengi huendesha wakiwa wamekunywa vileo hasa wakati wa usiku, ambapo hutumia vilevi vya aina mbalimbali.

Mara nyingi waendesha bodaboda wa usiku wanakunywa pombe kali zaidi ya chupa moja.  Wapo wengine wanaokunywa bia za kawaida katika kumbi mbalimbali za starehe wakiwa wanaendelea kusubiria abiria wanaotoka kustarehe wakati wa usiku waweze kiuwapeleka nyumbani.

Hali hiyo ilijidhirisha pale mwandishi alipotembelea klabu kubwa maarufu jijini Mwanza na kujionea waendesha bodaboda wakinywa pombe na wengine wakitumia ugoro huku wakisubiri abiria wao.

Wakati mwingine waendesha bodaboda hutumia mihadarati kama mbadala wa pombe kali ambazo hutoa harufu pale wanapozitumia.

Mwandishi alifanya mahojiano na baadhi ya waendesha bodaboda na viongozi wa vituo kumi vya bodaboda mkoani Mwanzo, ambao ni wasimamizi wa sheria za vituo hivyo ikiwemo marufuku ya kunywa vileo na kuendesha miongoni, ambapo walieleza bayana suala la tabia ya unywaji na uendeshaji lilivyo.

Athuman Rashid, ni mwenyekiti wa kamati tendaji ya umoja wa bodaboda wilaya ya Nyamagana, alisema kuna vijana ambao wamekuwa wakinywa na kuendesha kutokana na hulka zao wenyewe ijapokuwa elimu wamekuwa wakiitoa juu ya tabia hiyo ya unywaji.

“Hapa kwetu kulikuwa na vijana wengi waliokuwa wanaendesha huku wakiwa wamekunywa.  Na kuna kijana mmoja ambaye yeye alikuwa ana tabia ya kuendesha akiwa amekunywa tu yaani asipokunywa anakwambia hawezi kuendesha.”

“Sasa tulikuwa tunajiuliza sana kwanini yuko namna ile au ni tabia yake tu ambayo amejizoeza?  Tuliamua kumuonya baada ya kupata ajali akawa amejirekebisha.  Nadhani sasa ameacha. Ila sisi kama viongozi tunajitahidi kutoa elimu juu ya suala hili zima la ulevi ijapokuwa wapo wanaotusikia na kutuelewa na wengine hawaelewi kabisa,” alisema.

Renatus Francis ni mwendesha bodaboda kituo cha Masai darajani ambapo panatajwa kuwa mashuhuri kwa uuzaji wa vilevi mbadala wa viroba mathalani ugoro, alisema wapo waendesha bodaboda wawili, watatu wanaokunywa na kuendesha na wamewahi kupata ajali walipokaguliwa mifukoni walikutwa na chupa zenye pombe.

“watu wanatumia vilevi kama vile bia.  Serikali ilipiga marufuku pombe za viroba.  Lakini zimekuja pombe zingine zikiwa katika chupa ndogo ambazo kuna baadhi ya madereva ambao ni wanywaji wanavitumia,” alisema.

Mwandishi aliamua kuvinjari eneo hilo la Masai darajani ambalo ni maarufu kwa biashara ya ugoro, ambapo alijionea vijana wengi waendesha bodaboda wakimbilia kununua ugoro uliofungwa katika vifungashio vya karatasi na vikiuzwa kuanzia shilingi 500 mpaka 1000.

Maeneo mengine maarufu kwa uuzaji wa ugoro jijini Mwanza aliyoyatembelea mwandishi na kuona waendesha bodaboda wakipatiwa huduma hiyo ya ulevi huo ni Milongo kwa Kayese, Ofisi za zamani za stendi ya mabasi ya Tanganyika,  na Station karibu na Ofisi za Idara ya Uhamiaji.

Sebastian Leonald, ni dereva bodaboda kituo cha Bugando hospitalini, ambaye mwandishi alimshuhudia kwa macho akitumia ugoro wakati akiwa kazini na alipomuuliza kama anajua endapo sheria hairuhusu alisema kuwa hajui kama ugoro una madhara ndiyo maana unauzwa hadharani na serikali inajua.

”Ugoro sidhani kama unakatazwa kwasababu hata ukishuka hapo chini unauzwa tu na wamasai kwa shilingi 500.  Kwahiyo ugoro siyo kiroba.  Nafikiri kama ungekuwa na madhara basi serikali ingekuwa imeshapiga marufuku,” alisema.

Ugoro ni tumbaku iliyosagwa na kuwa unga.  Watu huitumia kwa kuvuta unga wake puani na wengine kubwia kwa kuweka katika mdomo wa chini.

Katika ugoro kuna kemikali ambayo kitaalamu inafahamika kama nikotini ambayo ni hatari kwa afya ya binadamu kwani husababisha maradhi mbalimbali ikiwemo; maradhi ya moyo, saratani,upungufu wa nguvu za kiume, mapafu na mengineyo mengi.

Kwa mujibu wa shirika la Africa Tobacco-Free Initiative ambalo linajihusisha na shughuli ya kudhibiti matumizi ya tumbaku nchini ikiwemo matumizi ya ugoro, tumbaku imekuwa ikiathiri afya za wananchi ambapo takribani watanzania 6,800 hupoteza maisha kila mwaka kutokana na maradhi yanayosababishwa na matumizi ya tumbaku kama vile kuvuta sigara na ugoro.

Godfrey Samwel ni mwendesha bodaboda kituo cha Mwanza hotel ambaye Julai 3, mwaka huu alipata ajali wakati akijaribu kulipita gari lililokuwa mbele yake lakini ghafla alikutana uso kwa uso na gari iliyokuwa inakuja kwa mbele yake.  Alipojaribu kuikwepa alijikuta akiyumba na kudondoka kutokana na mwendokasi aliokuwa nao, hali iliyomfanya kupata majeraha makubwa sehemu za kichwani na kupoteza fahamu papo hapo.

Samwel alipelekwa hospitali ya Mkoa wa Mwanza, Sekou Toure akiwa hajitambui ambapo alizinduka baada ya siku mbili.  Vipimo vya daktari vilivyoandikwa katika karatasi yake ya matibabu vilionyesha wazi kuwa alikuwa akiendesha huku akiwa amelewa, jambo ambalo liliweza kumsababishia ajali hiyo. 

Kutokana na majeraha aliyoyapata sehemu za kichwani imemfanya kupoteza kumbukumbu mara kwa mara.

Wakati akizungumza na mwandishi, Samwel alikiri kutumia pombe mara kadhaa ijapokuwa alisisitiza kuwa siyo wakati wote lakini pia imekuwa ni tabia kwa waendesha bodaboda wengi wanaokesha usiku wakifanya shughuli hiyo.

“Kwakweli huwa nakunywa lakini siyo sana.  Sasa mtu unakunywa bia mbili unaweza kusema mimi mlevi.  Kuna watu wanakunywa hata bia saba.  Hao ndio walevi.  Kwenye kituo chetu walio wengi wanakunywa. Katika kituo chetu tuko zaidi ya 30 lakini wasiotumia ni kama wawili tu,” Alisema Samwel.

Naye Makoye Kayanda, mwenyekiti wa umoja wa waendesha bodaboda mkoa wa Mwanza alisema serikali imedhibiti uuzaji wa viroba lakini bado kuna changamoto ya pombe mpya zinazofungashwa katika chupa ndogo ambazo huuzwa na kutumiwa na baadhi ya bodaboda walevi ijapokuwa viongozi wamekuwa wakifanya ukaguzi kugundua wanaoendesha wakiwa wamekunywa.

“Kwanza naomba nikiri wazi kuwa wapo baadhi ya waendesha bodaboda ambao wana tabia ya kulewa.  Tunaishukuru serikali sana kwa kuzuia uuzaji wa pombe ya viroba kwani bodaboda wengi walikuwa wanatumia sana.  Mbaya zaidi kwenye vituo vya bodaboda na daladala ndiko ambako kulikuwa na kibanda cha kuuza viroba.”

“Jambo ambalo bado linatusumbua kwa sasa ni waendesha bodaboda wa usiku.  Sisi kama viongozi tunafanya ukaguzi nyakati za mchana wote mpaka usiku saa nne au saa tano usiku.  Lakini tukiondoka tu, usiku wa manane ndio bodaboda wengi hunywa pombe na kutumia vilevi vingine,” alisema.

Kamanda wa kikosi cha usalama barabarani Mkoa wa Mwanza, SSP Robert Hussein alisema kuna tabia ya unywaji na uendeshaji kwa waendesha bodaboda na jeshi linajitahidi sana kudhibiti hali hiyo kwa kutumia vifaa ambavyo wanavyo askari kwa kufanya ukaguzi na kugundua madereva wanaolewa na kuendesha.

“Changamoto kubwa imekuwa ni ukamataji, ambapo bodaboda wengi wamekuwa wakikwepa kwa makusudi na pengine kuweza hata kusababisha ajali nyingine kwa kumgonga askari mkamataji au mtumiaji mwingine wa barabara,” alisema.

Wakili mkuu mfawidhi katika ofisi ya Mwanasheria mkuu wa serikali mkoa wa Mwanza, Seth Mkemwa, alisema kuwa sheria ya usalama barabarani imekuwepo kwa muda mrefu tangu enzi za ukoloni ingawa imekuwa ikifanyiwa mabadiliko kadhaa.  Lakini inabidi ipitiwe upya tena ili kuweka makali katika adhabu ambazo zinapaswa kutolewa kwa mtu atakayetiwa hatiani ili asiweze kurudia tena tofauti na ilivyo sasa.

“Kabla ya kufanyiwa marekebisho sheria ya mwenendo wa makosa ya jinai ya mwaka 1985, makosa yaliyokuwa yanasababisha vifo iwe barabarani au eneo lolote lile, aliyesababisha kifo alikuwa anafunguliwa kesi ya mauaji na akipatikana na hatia alikuwa anahukumiwa kama muuaji kwa kifungo maisha jera au hata kunyongwa wakati mwingine.”

“Lakini leo hata kama dereva ataua watu 30 kwa uzembe wake binafsi, akifikishwa mahakamani na kutiwa hatiani basi sheria itamuhukumu kifungo kisichozidi miaka mitatu tu.  Huu ni udhaifu mkubwa na inafanya madereva wengi kuendelea kufanya uzembe wanapokuwa barabarani,” alisema.

Meneja mkuu wa kanda ya ziwa ofisi ya mkemia mkuu wa serikali, Bonaventure Masambu alisema jeshi la polisi kwa sasa lina vifaa ambavyo linavitumia kupima kiwango cha pombe kwa madereva wanaokunywa, hivyo hawapokei sampuli kwa ajili ya kupima pombe.

Alisema kuna madereva wanaofikishwa kwa ajili ya kupimwa kiwango cha matumizi ya dawa zingine za kulevya kama vile mirungi, bangi, cocaine na heroine ambapo wengi wao wanabainika kutumia dawa hizo.

 “Kwenye dawa zingine za kulevya tunaendelea kupata kesi nyingi ambazo tunapima sampuli na kubaini wanaotumia dawa hizo. Miaka miwili iliyopita watu takribani 7237 tuliwapima na kubaini kuwa watu asilimia 9.33 wanatumia mirungi, asilimia 76.27 wanatumia bangi, asilimia 0.08 wanatumia cocaine, asilimia 14.07 wanatumia heroine, asilimia 0.18 wanatumia heroine na bangi kwa pamoja , asilimia 0.04 wanatumia mirungi na heroine kwa pamoja, watu 0.03 wanatumia mirungi na bangi kwa pamoja,” alisema.

Akifafanua zaidi madhara ya dawa za kulevya, Masambu, alieleza kuwa mtu akinywa pombe au dawa za kulevya humfanya ashindwe kumudu kuendesha vizuri chombo cha moto na wakati mwingine anaweza kusinzia.  Hivyo akiwa katika usukani anaweza kujikuta anapeleka gari pembeni, kugonga watembea kwa miguu, magari mengine, nyumba, au hata nguzo. 

“Kwa kawaida pombe ikizidi sana mwilini inaweza kuathiri uwezo wa kufanya maamuzi kwa mtu hasa pale anapokuwa akiendesha chombo cha moto.  Vilevi vingine kama vile bangi, heroin, mandrax vinamfanya mtu aweze kuona vitu visivyokuwa halisi kitaalamu tunaita ‘illussions’.  Mtu anaweza kuona simba kumbe ni mbwa.  Mtu anaweza kuona shimo kubwa kumbe ni kikorongo kidogo cha kawaida tu,” alieleza.

Sheria ya kupambana na kudhibiti dawa za kulevya ya mwaka 2015 (The Drugs Control and Enforcement) inatoa adhabu ya faini isiyopungua shilingi milioni 50 na isiyozidi milioni 500 au kifungo kisichopungua miaka 7 na kisichozidi miaka 30 au vyote kwa pamoja kwa mtu atakayebainika kujihusisha na uzalishaji wa dawa za kulevya mfano bangi au mirungi.

Ajali za bodaboda zimekuwa zikigharimu maisha ya vijana wengi kwa kutokuzingatia sheria ikiwemo kunywa vileo na kuendesha.  Hospitali ya rufaa Bugando inapokea majeruhi wa ajali watatu mpaka wanne kwa siku ambao huhitaji matibabu ya dharura na muda mrefu.

Waendesha bodaboda wengi wao hawana bima ya afya, hivyo wanapopata ajali hujikuta wakiuza mali zao kwa ajili ya kujigharamia matibabu.  Wapo ambao hushindwa kabisa kumudu gharama za matibabu hatimae kupewa msamaha na hospitali.
 
Mfano hospitali ya Bugando inatoa msamaha wa madeni ya matibabu takribani milioni tano mpaka 12 kila wiki kwa wagonjwa waliofikishwa hospitalini hapo kutokana na ajali za bodaboda, ambao wanakuwa wameshindwa kulipa gharama za matibabu zinazohitajika.

Afisa uhusiano wa hospitali ya Bugando, Lucy Mogele, alisema kuwa majeruhi wa ajali aliyeumia vibaya sana hususani bodaboda hulazwa kwa muda usipungua mwezi mmoja mpaka miezi sita na pengine mwaka mzima, jambo ambalo huongeza gharama mbalimbali kwa mgonjwa ikiwemo matibabu na huduma zingine.

“Gharama za kutibu majeruhi aliyeumia sana ni kubwa kutokana na ukweli kuwa hukaa sana hospitalini.  Kwa muda wote huo hupatiwa huduma za matibabu na huduma nyingine muhimu kwa mgonjwa kama vile chakula.”

“Mara nyingi wagonjwa wanaotibiwa hapa hujikuta wanadaiwa kuanzia laki nane mpaka milioni mbili.  Hii pia inategemea na muda.  Kuna wanaokaa mpaka mwaka hospitali.  Hawa gharama hukua zaidi,” alisema Mogele.

Kwa mujibu wa daktari bingwa wa mifupa hospitali ya Bugando, Dk. Isidor Ngayomela, alisema kwamba, “kiutaratibu kila unapoumia mfupa mmoja kitaalamu tunaita ‘region’ unahitaji huduma ya oparesheni moja kamili.  Hii ni tofauti na huduma ya oparesheni kwa idara zingine.”

“Kwahiyo kama umeumia ‘region’ moja ya mfupa hiyo ni oparesheni moja inayojitegemea pamoja na gharama zake.  Mgonjwa kama kaumia mifupa mitatu inamlazimu alipe mara tatu.  Katika hospitali yetu ya Bugando oparesheni moja inagharimu shilingi 320,000” alisema Dk. Ngayomela.

Kwa upande wa abiria wa bodaboda wao walisema kuwa usafiri wa bodaboda ni mzuri kwani umekuwa ukiwawahisha katika shughuli zao lakini changamoto imekuwa ni uhakika wa usalama wao.  Suala hilo limekuwa likichangiwa na uendeshaji wake, ambapo waeendesha bodaboda wamekuwa na mwendo mkali huku wengine wakionekana wamekunywa.

Getrude James, mkazi wa Makoroboi Mwanza alisema kuwa, “kuna watu wangu wa karibu ambao walipata ajali za bodaboda.  Mmoja alipata ajali akavunjika mguu na kuwekewa vyuma.  Mwingine yeye alivunjika meno.  Ajali hizi zilitokana na mwendo mkali wa bodaboda.   Kwahiyo mie naogopa sana kupanda mpaka leo,”

Fetrisha Bigaye, mkazi wa Igogo Mwanza alisema changamoto ya mwendokasi kwa waendesha bodaboda wengi imemfanya kutafuta bodaboda moja ambayo akiwa anashida ya kwenda mahali inamchukua kumpeleka na kumrudisha.

“Usafiri wa bodaboda ninautumia hasa ninapokuwa na kazi zangu za haraka nikiwa kama mama lishe.  Isitoshe ni nafuu sana na unaweza kukuwahisha mahali unapokwenda.   Nina bodaboda wangu maalumu wanaonipeleka na kunirudisha mahali ninapotaka.”

“Kuna siku nimewahi kupanda bodaboda tofauti kwasababu hawakuwepo ndiyo siku ambayo nilipata ajali na kuumia mguu, ambapo ilinigharimu kiasi cha shilingi 10,000 na yeye wala hakunichangia kwa lolote,” alieleza Bigaye.

Sheria ya usalama barabarani ya mwaka 1973 kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002 kifungu cha 44, inaeleza kuwa ni kosa la jinai kwa dereva yeyote kuendesha au hata kujaribu kuendesha akiwa amekunywa au kutumia dawa za kulevya.

Taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Kamanda wa kikosi cha usalama barabarani mkoa wa Mwanza, Julai 19, mwaka huu, inaeleza kuwa katika kipindi cha miaka mitano iliyopita kumekuwepo na ajali za barabarani zipatazo 1,540, ambazo zinajumlisha bodaboda na magari kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo unywaji na uendeshaji.

Ikifafanua zaidi taarifa hiyo ilisema kuwa katika kipindi cha miaka mitano iliyopita yaani kuanzia mwezi januari mpaka disemba 2012 mpaka 2016 kulitokea jumla ya ajali 1,540.

Takwimu za taarifa hiyo zinaonyesha mwaka 2012 kulikuwa na ajali asilimia 34.5, 2013 asilimia 21.5, 2014 asilimia 17.7, 2015 asilimia 13.3 na 2016 asilimia 12.6, asilimia 51 kati ya ajali hizo zilikuwa ni ajali za vifo, asilimia 40 ajali za majeruhi na asilimia 9 zilikuwa ni ajali za kawaida.

Hata hivyo jeshi la polisi kikosi cha usalama barabarani linafanya jitihada kubwa za kusimamia sheria ya usalama barabarani kwa kutoa elimu kwa makundi yote ya watumiaji wa barabara, kushirikiana na watunga sheria ili zitungwe sheria kali zaidi zinazokwenda na wakati, kukamata wanaovunja sheria kwa kufanya doria na misako pamoja na kupima ulevi miongoni mwa madereva katika maeneo mbalimbali ya jiji la Mwanza.

Mwenyekiti wa Taasisi ya mabalozi wa usalama barabarani nchini (RSA), John Seka, alisema nchi nyingi zilizoendelea zimekuwa na kampeni maalumu pamoja na matangazo mengi ya usalama barabarani, hali inayoleta mwamuko katika jamii.

Alisema hapa nchini kuna tatizo la usimamizi wa jeshi la polisi kikosi cha usalama barabarani, kwani bado halijaweza kujitosheleza kwa rasilimali kama vile vifaa vinavyopima ulevi na askari wa kudhibiti tabia hiyo kwa mdereva katika maeneo mbalimbali ya barabara.

“Usalama barabarani bado una changamoto.  Kuna askari wachache wa usalama barabarani na wengi wao hawana vifaa vinavyotosheleza katika ukaguzi na upimaji wa vileo kwa madereva,” alisema.
UCHUNGUZI: MADEREVA WA BODABODA MWANZA WENGI NI WALEVI UCHUNGUZI: MADEREVA WA BODABODA MWANZA WENGI NI WALEVI Reviewed by Unknown on 15:57 Rating: 5

No comments:

Theme images by merrymoonmary. Powered by Blogger.