MWANANYAMALA INAVYOLIA NA UHABA WA MADAKTARI WA MIFUPA


Na Mtapa Wilson
Hospitali ya Mwananyamala inakabiliwa na upungufu wa madaktari bingwa wa mifupa, jambo ambalo limekuwa likisababisha usumbufu kwa wagonjwa wa mifupa ikiwemo majeruhi wa ajali za barabarani, ambao wamekuwa wakifikishwa hospitalini hapo wakihitaji huduma ya matibabu ya mifupa.

Mganga mkuu wa hospitali hiyo, Nkungu Daniel, alisema kuwa hospitali yake imekuwa ikipokea wagonjwa wengi wa mifupa hususani majeruhi wa ajali mbalimbali za barabarani kuanzia watatu mpaka watano katika siku za kawaida na majeruhi watano mpaka 10 katika siku zenye mlundikano wa watu kama vile sikukuu, lakini changamoto kubwa imekuwa ni kukosekana kwa wataalamu wa mifupa wanaoweza kuwahudumia wagonjwa hao.

Alisema Mwanyanala imekuwa ikitoa huduma kwa majeruhi wa ajali za barabarani ambao wanakuwa hawajajeruhiwa vibaya sana katika mifupa ya miili yao kwa kuwapima na mashine za X-rays, kuwashona na kuwapatia dawa muhimu, ambazo zinawasaidia kupunguza maumivu na kutibu sehemu zilizoathirika na majeraha ya ajali.

“Kwa sasa tuna uwezo wa kutibu majeraha madogo madogo tu ya majeruhi wa ajali za barabarani kama vile michubuko, kuteguka na kuhama mifupa.  Lakini bado hatujawa na uwezo wa kutibu majeraha makubwa kama vile majeraha ya kichwa na kuvunjika mifupa kutokana na kukosa wataalamu wa mifupa katika hospitali yetu,” alisema Dk. Daniel.

Kadhalika Dk. Daniel alisema kuwa hospitali yake pia inakabiliwa na upungufu wa mashine za vipimo vya wagonjwa wa mifupa hususani majeruhi wa ajali katika sehemu za vichwa, jambo ambalo linawalazimu kupeleka wagonjwa wenye majeraha makubwa kichwani katika Taasisi ya Mifupa ya Muhimbili (MOI), ambapo wanaweza kupata vipimo na tiba bora zaidi.

“Kwakweli sasa hivi tuna vipimo vya X-rays peke yake, ambacho ni kipimo cha kuangalia majeraha ya kawaida tu ndani mwili wa majeruhi lakini haiwezi kupima majeraha yaliyoko kichwani.  Hii ni changamoto kubwa kwetu kwakuwa tunalazimika kuwaelekeza wagonjwa kutafuta vipimo vya city scan nje ya hospitali yetu kisha ndio tuwatibu,” aliongeza Dk. Daniel.

Aidha Dk. Daniel alisema kuwa mbali na changamoto ya ukosefu wa wataalamu wa mifupa na vifaa tiba kama vile vipimo vya city scan, bado kumekuwepo na changamoto ya kukosekana kwa wahuduma wa afya wakati wa usiku kutokana na ukweli kwamba kuna ajali nyingi zinatokea usiku na wagonjwa wanapofikishwa hospitalini hapo wanakuta wahudumu wakiwa wachache.

Kwa upande wao majeruhi waliofikishwa katika hospitali hiyo wameiomba serikali kuboresha zaidi huduma za afya katika hospitali za umma hususani kuajili wataalamu wa kutosha kwa ajaili ya kuhudumia wagonjwa wa mifupa.

Mathias Lucas, ni dereva wa bodaboda ambye ni muathirika wa ajali wa ajali za barabarani alisema kuwa kwa sasa hospitali inajitahidi kutoa huduma kwa majeruhi wa kawaida wa ajali lakini imekuwa ni ngumu sana kutoa huduma kwa watu waliojeruhiwa vibaya kutokana kukosa wataalaamu. 

Hivyo ameiomba serikali kuongeza wataalamu watakaosaidia kutatua changamoto hiyo hospitalini hapo.

Changamoto hiyo ya upungufu wa madaktari pamoja na vifaa tiba katika hospitali ya Mwananyamala imekuwepo pia katika hospitali ya Bugando jijini Mwanza ambayo ina madaktari bingwa wa mifupa watano pekee.

Madaktari hao hutoa huduma hospitalini hapo pamoja na hospitali zingine za kanda ya ziwa yenye watu takribani milioni 16 kupitia mpango wake wa kutembelea hospitali za mikoa na wilaya nyingine (Outreach programs).

Hali kama hiyo inaikabili hospitali ya wilaya ya Karatu jijini Arusha, ambayo ina uwezo wa kuhudumia majeruhi watatu tu katika kitengo chake cha dharura, jambo linawalazimu kusitisha huduma katika vitengo vingine vya hospitali ili kuongeza nguvu katika kitengo cha dharura.

Mathalani hali hii iliweza kujitokeza pale ajali mbaya ya basi aina ya costa, mali ya shule ya Lucky Vincent ya Jijini Arusha ilipoacha njia na kutumbukia katika mto Merera ulipo kwenye milima ya Rhotia na kuuwa wanafunzi takribani 32, walimu wawili na dereva wao mmoja.

Kwa mujibu wa Daktari kiongozi wa hospitali hiyo, Asanteli Makyao ni kwamba hospitali ya wilaya ya Karatu ina uhaba wa vifaa katika kitengo cha dharura kinachoshughulikia matukio ya ajali, huku ikiwa na watumishi wachache wa afya.

Hospitali ya wilaya ya Karatu ina watumishi wa afya 146 tu wakati inahitaji watumishi angalau watumishi 245 ili iweze kukidhi ombwe watumishi iliyonao katika kutoa huduma za dharura ikiwemo ajali.

Vilevile hospitali ya wilaya ya Karatu inakabiliwa na ukosefu wa vifaa muhimu katika kitengo cha dharura. Hivyo, hospitali hiyo haiwezi kutibu mtu aliyevunjika mfupa mkubwa wa mguu, aliyeumia kichwani au uti wa mgongo, jambo linaloilazimu kuwapa rufaa ya kwenda hospitali ya mkoa wa Arusha ya Mount Meru majeruhi wote wa ajali walioumia kiasi hicho.

Daktari bingwa wa upasuaji katika hospitali ya Mount Meru, Iddy Zubery anasema kitengo cha dharura katika hospitali hiyo kina uwezo wa kupokea majeruhi angalau 10 na kuwapa huduma kwa wakati mmoja.

Hata hivyo, Dk. Zubery nasema kumekuwepo na changamoto kadhaa kama vile ukosefu wa  mashine za kusaidia kupumua, hali inayosababisha baadhi ya majeruhi wa ajli kupewa rufaa ya kwenda hospitali ya KCMC Moshi mkoani Kilimanjaro.

Muuguzi katika huduma za dharura hospitali ya Mount Meru, Simphorosa Silalye anasema mara nyingi majeruhi wa ajali za barabarani hupata matatizo katika mfumo wa kupumua.  Hivyo huihitaji mashine za kisasa kwa ajili ya kuwasaidia kupumua tofauti na sasa ambapo bado kuna vifaa duni vya kusaidia kupumua vinatumika kama vile ‘Bag valve’.

Kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Afya Duniani (W.H.O) mwaka 2015, asilimia 50 ya vifo vyote vinavyotokana na ajali za barabarani  huwakumba watembea kwa miguu, waendesha baiskeli na bodaboda, ambapo vifo vya watembea kwa miguu ni asilimia 22, waendesha kwa miguu asilimia 5 na waendesha bodaboda ni asilimia 23. 
MWANANYAMALA INAVYOLIA NA UHABA WA MADAKTARI WA MIFUPA MWANANYAMALA INAVYOLIA NA UHABA WA MADAKTARI WA MIFUPA Reviewed by Unknown on 04:58 Rating: 5

No comments:

Theme images by merrymoonmary. Powered by Blogger.