ECOWAS, EAC NA SENEGAL NI WALE WALE?


Aliyekuwa Rais wa Gambia, Yahya Jammeh
Na Yusufu Lulungu

Nilihifadhi maoni yangu nikisubiri Dikteta Yahya Jammeh, anayeshutumiwa kuua hovyo (killing spree) na kutesa aondoke kwanza madarakani. Kwa upande wangu hata kama angeshinda uchaguzi bado ningependa ang'olewe tu kwakuwa hakuna demokrasia ya kuua na kutesa.

Namshukuru Mungu! Jammeh kakubali yaishe ila nimecheka kusikia Dikteta huyo anasema ni bora aondoke kwani hapendi kuona damu ya mtu ikimwagika, bila shaka kwa sasa ingekuwa damu yake.
Nije hapa kwenye kile kinachoitwa Senegal imelinda Demokrasia na EAC ni dhaifu ukilinganisha na ECOWAS.

Ni kweli Senegal ni mwanademokrasia? Hivi siku mathalani Rais Muhmoudu Buhari wa Nigeria akishindwa uchaguzi halafu akang'ang'ania madaraka, Senegal na ECOWAS watapeleka majeshi? tuache hilo.

Februari 1982 Senegal na Gambia ziliungana na kuunda shirikisho lililoitwa Senegambia.
Muungano ambao taifa la Gambia liliuingia huku likiwa na wasiwasi ambapo gazeti la The New York Times la Februari 1, 1982 likiwa na kichwa cha habari 'Gambia yaungana na Senegal huku ikiwa na wasiwasi (Gambia enters Union with Senegal on wary note), lilimnukuu Waziri Mkuu wa zamani wa Gambia, Mamadou Dia akisema shirikisho hilo ni unyang’anyi (annexation) na kuanzisha kampeni ya kulipinga.

Wananchi wengi wa Gambia walilipinga wakisema kuwa lingeimeza nchi hiyo kiuchumi, kisiasa nakadhalika.  
Na wakati huo wakiungana, nchi ya Gambia ilikuwa na watu takribani milioni 6, huku Senegal watu milioni 60.

Senegal ilikuwa na wabunge 100, Gambia wabunge 43 hii ni kwamba theluthi mbili ya wabunge ingetoka Senegal, hivyo Senegal ingekuwa na ushawishi kubwa kwa kila jambo na huenda mambo yao ndio yangepata nguvu bungeni.

Pia Senegal ikiwa na ukubwa mara 17 ya Gambia iliungana na jirani yake huyo kutokana na ushawishi wa Rais Abdou Diouf kwa Rais Dawda Jawara wa Gambia.

Gia kubwa aliyoitumia Rais Diouf kwa Rais Dawda ilikuwa ni suala la usalama kuwa nchi hizo zilikuwa kwenye kitisho cha uslama kutoka kwa Rais wa zamani wa Libya Kanali Muammar Ghaddaf ambae alishutumiwa kupanga mapinduzi ya kumuondoa madarakani Rais Dawda hapo July 1981 wakati Rais huyo akiwa London.

Ni nchi ya Senegal ambayo ilipeleka majeshi 2000 nchini Gambia ili kuzima jaribio hilo la mapinduzi, na jaribio likafa.  
Na hapo ndio ikawa rahisi Senegal kuishawishi Gambia kuunda shirikisho.
Ila kutokana na baadhi ya watu kupinga na baadhi ya mambo kutokaa sawa, Shirikisho hilo likafa hapo mwaka 1989.

Pamoja na kufa ila jitihada zikaendelea kufanyika ili kulifufua.  Pigo lilikuja mara baada ya Rais Dawda kupinduliwa na Rais Jammeh kuingia madarakani hapo mwaka 1994.

Rais Jammeh hakuonekana kulipa kipaumbele suala la shirikisho.  Na kuanzia mwaka huo (1994) Senegal ikaanza 'beef' na kuwa na tabia ya kuufunga na kuufungua mpaka (border) baina yake na Gambia likiwemo suala la ushuru wa forodha.

Nchi hizo zikaishi katika malumbano ya hapa na pale mpaka leo.  Mathalani katika mapinduzi ya hapo Desemba mwaka 2014 yaliyolenga kumpindua Jammeh ambae alikuwa nje ya nchi na mapinduzi hayo kushindwa, Rais Marky Sall alishutumiwa na Jammeh kuwa nyuma ya mapinduzi hayo.

Rais Jammeh na Sall wamedumu katika kushutumiana kwa muda.  Hivyo kitendo cha Jammeh kukubali na kukataa Matokeo ya Uchaguzi mkuu hapo mwaka jana ndio kikawa kimetoa njia ya Senegal kumuadhibu adui yake Jammeh.

Kwa mtindo huu sioni Demokrasia ya Senegal zaidi ya kusukumwa na dhamira ya uadui japo pia limefanya jambo jema.  Pia ECOWAS imekuwa na nguvu kwa kuwa Jammeh hakuwa kipenzi cha nchi nyingi za huko Afrika Magharibi na hata Ulaya, ikumbukwe kuwa hapo mwaka 2013 Jammeh aliiondoa nchi yake kwenye Jumuiya ya Madola, jambo ambalo liliiudhi Uingereza na washirika wake.

Naamini katika mazingira kama haya yakitokea Afrika Mashariki ipo siku mtu atagongwa tu.
Hebu jiulize kwanini Tanzania ilipeleka majeshi huko Goma Congo DRC kupambana na waasi wa M23 nasio waasi wa ADF, LRA, kwanini M23? Ukielewa hilo utafahamu ninachosema kuhusu EAC.
 
ECOWAS, EAC NA SENEGAL NI WALE WALE? ECOWAS, EAC NA SENEGAL NI WALE WALE? Reviewed by Unknown on 11:51 Rating: 5

No comments:

Theme images by merrymoonmary. Powered by Blogger.