MIKOA NANE YAFAIDIKA NA MIRADI YA VISIMA VYA KISASA

Mkuu wa Wilaya ya Same, Rosemary Senyamule (wakwanza kushoto) akifurahia pamoja na baadhi ya viongozi wa Serengeti Breweries Limited, mara baada ya uzinduzi wa mradi wa maji katika kijiji cha Makanya, mapema mwaka jana.
Na Mwandishi wetu, Dodoma

Ili kukabiliana na tatizo la uhaba wa maji katika maeneo mbalimbali nchini hususani vijijini, hali inayosababisha usumbufu kwa watoto wa kike kutembelea umbali mrefu kutafuta maji, kampuni ya bia ya Serengeti (SBL) imechimba visima 16 vya kisasa katika mikoa nane ili kuiwezesha jamii kupata maji safi na salama.

Msaada huo wa visima vya maji unakadiriwa kuwanufaisha takribani Watanzania milioni mbili katika maeneo hayo kwa kupata maji ya uhakika ikiwa ni sehemu ya mchango wa kijamii (social corporate responsibility) wa kampuni hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari leo mjini Dodoma, Mkurugenzi wa Uhusiano wa SBL, John Wanyancha, alisema kwamba msaada huo umejikita katika kupunguza uhaba wa maji katika maeneo ambayo kwa muda mrefu yamekuwa yakitaabika kutokana na uhaba huduma hiyo muhimu.

“SBL ina sera iliyojikita katika ustawi wa jamii yetu ambapo maji ni moja ya maeneo ambayo ni kipaumbele chetu na sera yetu imefafanua pia malengo yake ya kutoa msaada kwa jamii,” alisema.

Aidha Wanyancha alisema kuwa kwa kutoa huduma ya maji ya uhakika katika jamii inawawezesha wananchi kupata fursa zaidi ya kutumia muda mwingi kujikita katika shughuli za uzalishaji badala ya kupoteza muda kutafuta maji katika umbali mrefu.

Mikoa ambayo SBL imechimba visima hivyo ni Iringa, Dar es Salaam, Pwani, Kilimanjaro, Mwanza, Ruvuma, Tanga na Dodoma.  

Mpango wa hisani ya kusaidia jamii wa SBL kupitia program yake ya Maji kwa Uhai, kwa mwaka 2017 umelenga kuanzisha miradi ya maji zaidi katika maeneo ya Ngare Nairobi wilaya ya Siha (Kilimanjaro), Chang’ombe B wilayani Temeke (Dar es Salaam), Karatu na Likamba mkoani Arusha ambapo watu zaidi ya 300,000 watanufaika na miradi hiyo.


MIKOA NANE YAFAIDIKA NA MIRADI YA VISIMA VYA KISASA MIKOA NANE YAFAIDIKA NA MIRADI YA VISIMA VYA KISASA Reviewed by Unknown on 15:11 Rating: 5

No comments:

Theme images by merrymoonmary. Powered by Blogger.