SERIKALI ONDOA CHANGAMOTO KATIKA MFUMO WA ELIMU NCHINI

Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Prof. Joyce Ndalichako.
Na Mtapa Wilson

Kwa hapa tulipofikia, serikali inapaswa kupitia upya sera ya elimu nchini na kuisimamia ili kuhakikisha mfumo wa elimu hauyumbishwi kutokana na kiwango cha utashi wa mawaziri wanaokabidhiwa sekta hiyo muhimu kuelekea katika uchumi wa viwanda.

Tangu uhuru wa nchi yetu, mfumo wa elimu umekuwa unaamuliwa na matakwa ya Waziri wa elimu aliyeko madarakani, hali inayosababisha udhaifu mkubwa katika mfumo wa elimu, ambao huigharimu Taifa kwa kiasi kikubwa.

Takribani miongo mitano sasa, sekta ya elimu nchini imekuwa ikifanyiwa mabadiliko badala ya mapinduzi, ambayo yatasaidia kufikia dira ya maendeleo ya Taifa letu ikiwamo uchumi wa viwanda na pato la kati ifikapo 2025.

Tukirejea huko nyuma, Wizara ya Elimu imeongozwa na Mawaziri zaidi ya Watano, ambao kila mmoja alikuja na namna anavyoona inafaa kuwa.  Hali hii haihitaji kuvumiliwa tena kwani umefika wakati wa kuweka muafaka wa kitaifa katika mfumo wa elimu nchini, ambao utafuatwa na Mawaziri wote wanaochaguliwa kuongoza Wizara hiyo.

Baadhi ya mabadiliko yaliyoshuhudiwa yakitokea katika mfumo wa elimu nchini yamekuwa hayana mchango wenye tija katika mageuzi ya elimu badala yake yanarudisha nyuma jitihada za serikali kutaka kuboresha elimu nchini.

Tumeshuhudia mabadiliko kadha wa kadha mathalani, mdaraja ya ufaulu, mara daraja la tano, mara mfumo wa GPA, mara wanafunzi wa kidato cha nne kujiunga na chuo kikuu, hali inayopingana na miongozo ya udahili wa wanafunzi katika ngazi ya elimu ya juu nchini.

Upitiaji upya wa sera pamoja na kuweka sheria mpya ya elimu utasaidia kuboresha kiwango cha elimu nchini, jambo ambalo linaweza kufanikisha hata kuleta maendeleo ya Taifa kwa kutekeleza dira ya uchumi wa kipato cha kati na viwanda.

Kumekuwapo na changamoto kubwa ya sheria za elimu nchini ambazo zimekuwa hazirandani na sera ya elimu, hali inayosababisha kubadilika kwa sera za elimu kutokana na viongozi wanaoingia kuongoza na kutoka katika sekta ya elimu nchini kwa nyakati tofauti.

Endapo kutakuwa na sera ya elimu inayorandana na sheria ya elimu itasaidia kutekeleza dira ya maendeleo ya elimu nchini bila kujali kiongozi au mtu yeyote ambaye anaingia kuongoza sekta ya elimu bila kuathiri lengo la sera iliyopo.

Taifa letu limechukua muda mrefu sana bila kupitia upya sera na sheria ya elimu nchini.  Sheria ya elimu iliyopo sasa iliandikwa upya mwaka 1978 na kufanyiwa marekebisho mwaka 1995. 

Mwaka huo huo ndio kuliundwa sera ya elimu ambayo ilikuwa inafuata sheria ya elimu ya mwaka 1978. Lakini tangu mwaka huo, sheria ya elimu haijapitiwa tena ili kuweka mipaka ya mabadiliko ya elimu, ambayo inazingatia dira ya maendeleo ya Taifa ikiwemo kukua kwa uchumi.

Watumishi wa sekta ya elimu nchini pia wanapaswa kuzingatia hati idhini ya elimu inayotolewa na serikali, ambayo huwaongoza viongozi, wakuu wa idara, na wakurugenzi na watumishi wa Wizara ya elimu katika kutekeleza sera ya elimu.

Uzingatiaji huo utasaidia kuhakikisha kunakuwepo na fursa ya utoaji wa elimu bora katika ngazi zote za elimu yaani kuanzia elimu ya awali hadi Chuo Kikuu.

Licha ya udhaifu mkubwa uliopo katika mfumo wa elimu lakini bado kuna changamoto kubwa ya wanafunzi wa elimu ya juu kumudu kupata elimu hiyo kwakuwa hakuna kanuni wala kipimo maalumu cha utambuzi wa uwezo wa wanafunzi kujigharamia elimu yao ya juu, jambo ambalo linafanya wanafunzi wengi kukosa mikopo ya elimu inayotolewa na serikali kupitia Bodi ya Mikopo (HESLB).

Kutokana na kukosekana kwa kanuni na kipimo maalumu cha kutoa mikopo kwa wanafunzi wa vyuo vikuu nchini, kinachofanyika sasa ni ubashiri ambao kwa kiasi kikubwa ‘unawanyonga’ wanafunzi wengi ni watoto wa masikini na yatima ambao hawana mbele wala nyuma ambao hata kusoma shule za sekondari walifanikiwa kwa kupitisha mabakuli ya kuomba kwa ndugu jamaa na marafiki.

Mfumo giza uliopo Bodi ya Mikopo unatoa mianya ya rushwa katika upatikanaji wa mikopo, hali ambayo pia inachangia madhara makubwa ya kuendelea kuwa na tabaka la wasomi (wanomudu kujisomesha) na wajinga (wanaoshindwa kumudu kujisomesha) kwa kukosa haki yao ya msingi ya kupata elimu.

Serikali ina wajibu wa kubeba jukumu la kuwasomesha bure wanafunzi wote kuanzia shule ya msingi hadi vyuo vikuu ili kutengeneza Taifa la wasomi wasio na matabaka kati ya walionacho na wasionacho.

Nchi yetu sio masikini kiasi cha kushindwa kudhamini elimu ya wananchi wake.  Serikali ina uwezo wa kutenga rasilimali yeyote ambayo mapato yake yote yataelekezwa katika kudhamini elimu nchini. 

Haiwezekani leo mwanafunzi anayesoma bure kuanzia chekechea mpaka kidato cha nne, awe na uwezo kujigharamia ada ya Chuo Kikuu, ambayo ni wastani Shilingi milioni 1.5 kwa vyuo vya serikali.  Na ukiangalia katika vyuo vya binafsi ada inazidi hapo.


SERIKALI ONDOA CHANGAMOTO KATIKA MFUMO WA ELIMU NCHINI SERIKALI ONDOA CHANGAMOTO KATIKA MFUMO WA ELIMU NCHINI Reviewed by Unknown on 11:27 Rating: 5

No comments:

Theme images by merrymoonmary. Powered by Blogger.