WADAU WATAKIWA KUWEKEZA KATIKA RIADHA

Mshindi wa mbio za Standard Chartered Mumbai Marathon zilizofanyika nchini India, Alphonce Simbu (kulia) akiwa na Meneja wa Kitengo cha Mahusiano ya Umma wa Kampuni ya Multichoice Tanzania, Johnson Mshana, mara baada ya kuwasili chini hivi karibuni.

Na Mtapa Wilson

Serikali imesema kuwa uwekezaji mkubwa wa wadau katika tasnia ya michezo utasaidia kukuza na kuboresha hali ya michezo nchini, jambo ambalo linaweza kurudisha heshima na utukufu wa michezo mbalimbali katika Taifa letu ikiwemo mchezo wa riadha.

Akizungumza mbele ya waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam, wakati wa hafla ya kumpongeza mshindi wa mbio za Standard Chartered Mumbai Marathon, zilizofanyika nchini India, January 15 mwaka huu, Alphonce Simbu kutoka Tanzania, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye, alisema kuwa kwa muda mrefu sana Taifa limekuwa nyuma katika medani za michezo ya kitaifa na kimataifa kutokana na uwekezaji duni wa wadau katika michezo.

“Mafanikio ya Alphonce Simbu, kwa msaada wa Kampuni ya Multichoice Tanzania ni mfano mzuri kwamba kumbe tukiwekeza inawezekana.  Kwa muda mrefu Tanzania tumekuwa na maneno mengi sana na tabia ya kunyoosheana vidole sana.  Lakini kumbe ni uamuzi wa kuwekeza tu.

Multichoice Tanzania imewekeza kwa Simbu kwa muda usiozidi hata mwaka mmoja na matokeo yake tumeyaona.  Kupitia hadhara hii ninawaomba wadau wa sekta binafsi kushirikiana serikali kuwekeza katika michezo, ambayo imekuwa na mvuto kwa watu, ili kutengeneza fursa ya kutangaza vivutio vyetu vya utalii lakini pia kuendeleza michezo nchini,” alisema Waziri Nape.

Kwa upande wake Simbu alisema kuwa amefarijika sana kuona mwitikio mkubwa wa Watanzania baada ya kuibuka mshindi mashindano hayo ya mbio, ambayo yalishirikisha wanariadha mbalimbali kutoka Mataifa yenye uzoefu na sifa za kujinyakulia ushindi katika mashindano ya kimataifa kama vile Kenya na Ethiopia.

“……mtaona kwenye 10 bora, kulikuwa na Wakenya 7, Waethiopia 2 na Mtanzania nilikuwa peke yang tu.  Hii inaleta ugumu sana kwenye mashindano tofauti na mkiwa wengi kwakuwa mnaweza kusaidiana mbinu ilimradi mwishoni ashinde mtu wa timu yenu.

Lakini pia nimefarika sana kuona watu wengi sana wakifuatilia maendeleo yangu ikiwemo serikali yangu ambayo ilinitumia pongezi dakika chache baada ya ushindi wangu kupitia Waziri wa Michezo.  Hii inaonyesha dhahiri kuwa hata yeye mwenyewe Waziri alikuwa akifuatilia kwa karibu sana mashindano hayo,” alisema Simbu.

Nae Kaimu Mkurugenzi wa Multichoice Tanzania, Ronald Shelukindo, alisema kuwa Multichoice Tanzania itaendelea kumdhamini Simbu, na kwamba wanatarajia kuwa atafanya vyema kwenye michuano ijayo ya London Marathon, Aprili, mwaka huu na ile ya Dunia itakayofanyika Agosti, mwaka huu.

“Tunaendelea kumdhamini Simbu kwa kushirikiana na Meneja wake na kocha wake pamoja na Mwalimu wake ili kuhakikisha kuwa anajinoa vizuri kwa ajili ya mashindano yanayomkabili mbeleni.

Tunataka Simbu awe chachu na hamasa kwa vijana wanochipukia katika mchezo wa riadha nchini.  Tunamuunga mkono ili aendelee kushinda na chipukizi wengine waone kweli inawezekana mtu kushinda na wala siyo kubahatisha,” alisema.
WADAU WATAKIWA KUWEKEZA KATIKA RIADHA WADAU WATAKIWA KUWEKEZA KATIKA RIADHA Reviewed by Unknown on 10:32 Rating: 5

No comments:

Theme images by merrymoonmary. Powered by Blogger.