SPIKA WA BUNGE ATANGAZA KUJIUZULU KWA WAZIRI WA MAGUFULI

Aliyekuwa Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Walemavu, Dk. Abdallah Possi akiapishwa mbele ya Rais John Magufuli, mara baada ya kuteuliwa kuwa Mbunge na Naibu Waziri mwishoni mwa mwaka 2015.
Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Ikiwa ni siku moja tu imepita tangu Rais John Magufuli kuwaapisha Mabalozi sita watakaoiwakilisha Tanzania katika nchi mbalimbali, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai, ametangaza kupokea barua ya kujiuzulu Ubunge, Dk. Abdallah Possi.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa leo na Kitengo cha Habari, Elimu na Mawasiliano, Ofisi ya Bunge inasema kwamba Dk. Possi aliwasilisha barua yake ya kujiuzulu kwa Spika Ndugai jana Januari 20, mwaka huu, mara baada ya kuteuliwa kuwa Balozi, ambapo atapangiwa baadae nchi ambayo atakwenda kuiwakilisha.

“Spika Ndugai anapenda kuwataarifu Wabunge wote na wananchi kwa ujumla kuwa jana tarehe 20 Januari, 2017, amepokea barua ya kujiuzulu Ubunge iliyowasilishwa kwake na Dk. Abdallah Possi, aliyeteuliwa kuwa Balozi katika kituo atakachopangiwa hapo baadae,” ilisema taarifa hiyo.

Taarifa hiyo iliongeza kuwa kufuatia barua hiyo ya kujiuzulu ubunge wa Dk. Possi, iliyozingatia masharti ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, ibara ya 67 (1) (g) ikisomwa pamoja na ibara ya 149 (1) (d), Spika Ndugai amemwandikia barua Rais Magufuli kuwa hivi sasa Wabunge wa kuteuliwa na Rais waliopo Bungeni ni saba na hivyo nafasi zilizo wazi ni tatu baada ya Dk. Possi kujiuzulu.

Wabunge waliokwisha kuteuliwa mpaka sasa ni Naibu Spika, Dk. Tulia Ackson, Waziri wa Elimu, Prof. Joyce Ndalichako, Waziri wa Fedha, Dk Philip Mpango, Naibu Waziri wa Fedha, Dk. Ashantu Kijaji, Waziri wa Ujenzi, Prof. Makame Mbarawa, Mhadhiri wa Sheria kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) Prof. Palamagamba Kabudi na aliyekuwa Mkuu wa Msafara wa Kampeni za Chama cha Mapinduzi (CCM) wakati wa uchaguzi mkuu mwaka 2015, El Hadji Abdallah Bulembo.

Dk. Possi aliteuliwa na Rais Magufuli kuwa Mbunge, ambapo baadae aliteuliwa tena kuwa Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Walemavu.


SPIKA WA BUNGE ATANGAZA KUJIUZULU KWA WAZIRI WA MAGUFULI SPIKA WA BUNGE ATANGAZA KUJIUZULU KWA WAZIRI WA MAGUFULI Reviewed by Unknown on 14:26 Rating: 5

No comments:

Theme images by merrymoonmary. Powered by Blogger.