FATMA MAGHIMBI, KIONGOZI WA KWANZA WA KAMBI RASMI YA UPINZANI NA MUASISI WA CUF ALIYEREJEA CCM




           

Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) wakati huo, Dk. Jakaya Kikwete akimkabidhi kadi ya chama hicho, aliyewahi kuwa Mkuu wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Fatma Maghimbi, baada ya kutangaza kuihama CUF na kujiunga na CCM, katika mkutano wa kampeni Kawe, Dar es Salaam, mwaka 2010.
Na Mtapa Wilson

Unapozungumzia waasisi wa vyama vya upinzani nchini huwezi kuacha kumtaja Fatma Maghimbi akiwa ni miongoni mwa wanawake wa kwanza kuingia katika ulingo wa siasa hususani siasa za vyama vya upinzani nchini ukiachilia mbali Elizabeth Kasembe na Ania Chaulembo.

Maghimbi aliingia katika siasa mwaka 1992 mara baada ya kuwa amehudumu vyema katika nafasi yake ya ujumbe wa sekretarieti katika tume ya maoni ya katiba chini ya aliyekuwa Jaji Mkuu wa Tanzania, Francis Nyalali ambapo maoni asilimia 20 ya watanzania walipendekeza Tanzania kuwa na mfumo wa vyama vingi na asilimia 80 ya watanzania walipendekeza Tanzania ibaki katika mfumo wa chama kimoja.

Licha ya matokeo hayo ya maoni ya yaliyokusanya na tume ya Nyalali, ili kuinua kutanua zaidi wigo wa maendelo ya kidemokrasia nchini ilishauriwa ni bora Tanzania iingie katika mfumo wa vyama vingi (Multipartism) ambao utaleta changamoto za kiuongozi badala mfumo wa chama kimoja ambacho hakiruhusu mawazo mbadala katika kufikia maendeleo yenye tija kwa wananchi wa kawaida.

Mara baada ya mfumo wa vyama vingi kuwa umeridhiwa ndipo vyama vingi vya upinzani viliundwa ikiwemo chama cha wanchi Cuf ambacho kilikuwa kikiongozwa na Mwenyekiti wake wakati huo James Mapalala kutoka Tanzania bara na katibu wake akiwa ni Shaban Khamis Mloo kutoka Zanzibar, wakati huo Maalim Seif Sharif Hamad akiwa Makamu Mwenyekiti wa Cuf.

Maghimbi alihamasika zaidi kujiunga na chama cha wananchi mara baada ya kushawishiwa na katibu wa chama hicho ambae ni marehemu kwa sasa, Shaban Mloo ambapo aliamua kuachana na kazi yake katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).

Akiwa tayari ameshaingia katika siasa alikumbana na changamoto mbalimbali ikiwemo kukumbana na pingamizi za mara kwa mara kutoka kwa serikali na wananchi kwa ujumla ambao walikuwa na mtazamo hasi dhidi ya vyama vya upinzani.  

Muda mwingine Maghimbi aliratibu mikutano ya kisiasa lakini mwisho wa siku kulikuwa na idadi ndogo ya wahudhuliaji jambo ambalo lilikuwa linakatisha tamaa lakini kamwe halikumkatisha tamaa katika harakati zake za mageuzi nchini.

Kutokana na harakati nyingi alizozifanya katika maeneo mbalimbali nchini, mwaka 1995 ulifanyika uchaguzi wa kwanza chini ya mfumo wa vyama vingi ambapo aligombea na kuibuka mshindi katika nafasi ya ubunge wa jimbo la Chakechake lililopo mkoa wa Pemba Kusini baada ya kumbwaga aliyekuwa mgombea wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Ramadhan Khamis Feruzi.

Kutokana na idadi kadhaa ya wabunge wa upinzani kuingia bungeni baada ya uchaguzi wa mwaka 1995, chama cha wananchi Cuf kilifanikiwa kuunda kambi rasmi ya upinzani bungeni ambapo Maghimbi alikuwa Kiongozi Mkuu wa kambi hiyo jambo lililomfanya kuweka rekodi kubwa mbili.  Kwanza, Maghimbi aliweka rekodi yakuwa Kiongozi Mkuu wa kwanza wa kambi rasmi ya upinzani bungeni tangu kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi. 

Rekodi ya pili aliyoweka Maghimbi ni kuwa mwanamke wa kwanza kushika wadhifa mkubwa (Kiongozi Mkuu wa kambi rasmi ya upinzani bungeni) tangu mfumo wa vyama vingi ulipoanza mwaka 1992.

Mara nyingi Maghimbi alionekana jasiri asiyetetereka wakati wote wa kuwasilisha hotuba yake kama Kiongozi Mkuu wa Kambi rasmi ya upinzani kwani hoja zake zilionekana kuwa na mashiko kutokana na utamaduni wa kufanya tafiti mbalimbali kabla ya kuwasilisha hotuba yake bungeni.
  
Licha ya kuwa Maghimbi alikuwa mwanamke, uwezo wake wa kujenga hoja katika hotuba zake ulifanya hotuba zake kuwagusa wengi kutokana na taarifa muhimu ambazo alikuwa akizitoa kwa umakini wa hali ya juu.

Kuna wakati hali ya upinzani ilikuwa kali bungeni kiasi cha wabunge wa chama tawala kuamua kumzomea wakati akiwasilisha hotuba yake.  Lakini bado alisimama kidete kutetea kile alichokiamini kwa niaba ya kambi yake rasmi ya upinzani bungeni ambayo ilikuwa inaundwa kwa kiasi kikubwa na chama cha wananchi Cuf.

Ilipofika katika uchaguzi wa mwaka 2000, Maghimbi alianguka katika nafasi yake ubunge jimboni mwake kutokana na kile kilichoitwa mbinu chafu za kisiasa za Chama cha Mapinduzi (CCM).  Alikaa nje ya bunge kwa kipindi cha miaka mitano ambapo mwaka 2005 alirejea tena kugombea kiti chake cha ubunge katika jimbo lake la Chakechake na kuibuka mshindi tena kwa mara nyingine.

Safari hii aliporejea bungeni ateuliwa na kambi rasmi ya upinzani kuwa Waziri kivuli wa Katiba, Sheria na Utawala bora (kwa wakati huo) ambapo alisimamia hoja kuu tatu katika nafasi yake.  Kwanza, alishinikiza serikali kufanya mabadiliko ya katiba.

Pili, Maghimbi aliwasilisha hoja bungeni ambayo ilikuwa ikiishinikiza serikali kufanya mabadiliko ya katiba yatakayoruhusu kuwepo kwa mgombea binafsi.

Vivile hoja ya tatu ya Maghimbi ilikuwa ni uanzishaji wa mahakama ya kadhi.  Hii  ilikuwa ni moja ya hoja ambazo alizinadi sana wakati akiwa Waziri kivuli wa Katiba kwa kipindi hicho ili kutoa mwanya kwa waumini wa dini ya kiislamu kudai haki zao katika misingi ya dini yao.

Mwaka 2010, ikiwa ni kipindi cha uchaguzi wa awamu ya pili ya uongozi wa Rais Jakaya Mrisho Kikwete, Maghimbi alishindwa kutetea nafasi yake ya ubunge katika hatua ya kura za maoni dhidi ya mgombea mwezie ndani ya chama, Haji Mussa Kombo.  Mwaka huo huo aliondoka chama cha wananchi Cuf na kuchukua kadi ya Chama cha Mapinduzi.

Wasifu wa Fatma Maghimbi

Fatma Kitwana Msalem ni mzaliwa wa Chakechake, mkoa wa Pembe kusini, visiwani Zanzibar.  Alizaliwa Desemba 10, 1946.  Ni mtoto wa mwisho kati ya watoto nane waliozaliwa na Mzee Kitwana Msalem.  Alipata jina la Fatma Maghimbi baada ya kuolewa na muwewe anayeitwa Mzee Mussa Maghimbi.

Alisoma elimu yake ya msingi katika shule ya msingi Madungu iliyoko Chakechake kuanzia mwaka 1952 mpaka 1958.  Akiwa darasa la sita alihamishiwa katika shule ya kikatoliki iliyokuwa ikifahamika kama ‘St. Joseph Convent Primary School’ iliyoko eneo la Wete ambapo alihitimu darasa la nane mwaka 1959.

Mwaka 1960, Maghimbi alijiunga na shule ya sekondari Sayyida Maduka iliyoko Unguja, mkoa wa Mjini Magharibi na kuhitimu kidato cha nne mwaka 1963.   Wakati akiwa katika harakati za kujiunga na masomo ya kidato cha tano na sita ndipo Mapinduzi ya Zanzibar, hali iliyomfanya Maghimbi ashindwe kuendelea tena masomo yake.

Kutokana na mapinduzi ya Zanzibar ya 1964, ambayo yalisababisha wazungu, wahindi na magoa waliokuwa wakifanyakazi katika ofisi za serikali kuacha kazi.  Huu ulikuwa mwanzo wa serikali ya Mapinduzi kuchukua baadhi ya wananchi wa Zanzibar na kuja kuwasomesha bara katika kozi maalumu za maofisini ili wakafanye kazi katika nafasi zilizokuwa zimeachwa wazi.

Katika mpango huo, Maghimbi nae alichukuliwa kuja kusoma kozi ya ukatibu mukhtasi (Secretarial Course) katika chuo cha ufundi Dar es Salaam (D.I.T kwa sasa) ambapo baadae alirejea visiwani Zanzibar na kwenda kuwa Katibu Mkuu wa Rais Abeid Amani Karume.   Hii nayo inamuweka katika rekodi ya kuwa Katibu Mkuu wa kwanza wa Rais wa kwanza wa Zanzibar.

Baada ya kuhudumu kwa muda miaka mitatu, mwaka 1968 Maghimbi aliolewa bara na Mzee Mussa Maghimbi ambaye alikuwa ni Mwalimu katika shule ya vipaji maalumu Kibaha iliyoko mkoa wa Pwani. 
Hali hii ilimlazimu Maghimbi kuondoka Zanzibar kuja kuishi bara na mumewe ambapo yeye alihudumu tena kama Katibu katika ofisi ya Mganga mkuu wa kituo cha elimu Kibaha ambacho kilikuwa chini ya mradi unaoendesha shule ya sekondari Kibaha, Kituo cha afya kibaha na Taasisi ya kilimo Kibaha.

Mwaka 1971, Maghimbi alihama kutoka Kibaha mpaka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambapo aliajiriwa kama Katibu wa chuo. Alihudumu hapo kwa takribani miaka kumi na tano ambapo alipata fursa ya kujiendeleza kielimu kwa masomo ya kidato cha tano na sita kupitia mpango maalumu wa Chuo Kikuu kuwandeleza wafanyakazi wake kielimu.

Kutokana na juhudi kubwa katika masomo yake ya kujiendeleza aliweza kufaulu vizuri mitihani yake mwisho.   Mwaka 1989 alijiunga na masomo ya juu kwa ngazi ya chuo kikuu akisomea sheria mpaka alipohitimu mwaka 1992.

Ikiwa ni mpango wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kubadilishana maarifa kwa kusomesha wafanyakazi wake katika vyuo vingine duniani, mwaka 1992, Maghimbi alipata ufadhili wa kwenda kusoma shahada ya uzamili katika Chuo Kikuu cha Warwick kilichopo Birmingham nchini Uingereza ambapo alihitimu mwaka 1993.

Aliporejea nchini aliendelea kufanya kazi Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) akiwa kama Afisa utawala wa sheria ambapo baadae alijiunga moja kwa moja na siasa za upinzani baada ya kuombwa na viongozi wa chama cha wananchi Cuf wakti huo.

Maghimbi ana watoto watatu ambapo kati yao wawili ni wakike na mmoja ni wa kiume.  Mtoto wake wa kwanza ni wa kiume ambae ni daktari wa binadamu, wa pili ni mtoto wa kike ambae ni Meneja wa huduma kwa wateja katika mfuko wa pensheni wa PSPSF, na mtoto wake wa mwisho ni Jaji wa Mahakama kuu kanda ya Arusha.
  
FATMA MAGHIMBI, KIONGOZI WA KWANZA WA KAMBI RASMI YA UPINZANI NA MUASISI WA CUF ALIYEREJEA CCM FATMA MAGHIMBI, KIONGOZI WA KWANZA WA KAMBI RASMI YA UPINZANI NA MUASISI WA CUF ALIYEREJEA CCM Reviewed by Unknown on 07:25 Rating: 5

No comments:

Theme images by merrymoonmary. Powered by Blogger.