MISAADA YA WAATHRIKA WA MVUA MWAKATA KUJENGA MIUNDOMBINU YA SERIKALI

Rais Jakaya Kikwete (wakatai huo) akiwapa mkono wa pole kina mama, ambao ni waathirika wa mvua ya mawe iliyonyesha katika Kijiji cha Mwakata, Wilaya ya Kahama, Mkoani Shinyanga mwanzoni mwa Machi, 2015.

Na Mtapa Wilson, Kahama

Serikali imechukua vifaa vya ujenzi vilivyokuwa vimekusanywa kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za waathirika wa vijiji vitatu vya Kata ya Mwakata wilayani Kahama, mkoani Shinyanga, ambavyo viliathiriwa vibaya na mvua kubwa ya mawe mwanzoni mwa Machi 2015, na kusababisha vifo vya watu 47 na wengine 112 kujeruhiwa.

Serikali imesema vifaa hivyo vya ujenzi vitaelekezwa kwenye ujenzi wa miundombinu ya serikali pamoja na miradi mbalimbali ya maendeleo ya serikali katika vijiji vitatu vya Magunhumwa, Mwakata yenyewe na kijiji cha Numbi.

Vifaa vya ujenzi vilivyochukuliwa na serikali kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa kile ilichokiita miundombinu ya serikali kama vile ujenzi wa shule, nyumba za walimu, ukarabati wa vyumba vya madarasa, na ujenzi wa ofisi za serikali za vijiji ni jumla ya tofali za saruji 33,365 na mabati 1,346.

Kwa mujibu wa Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Fadhili Nkurlu ni kwamba hatua hiyo imekuja kufuatia kauli ya Rais wa Tanzania, Dk. John Magufuli, aliyoitoa Julai 31, mwaka jana akiwa kata ya Isaka, Mkoa wa Shinyanga kuwa serikali haitalipa fidia kwa wananchi waliopatwa na maafa ya mvua iliyobomoa nyumba zao badala yake itajielekeza kutatua tatizo kubwa la uhaba wa maji.

“Serikali haiwezi ikajenga Mwakata kama alivyosema Mheshimiwa Rais.  Tofali hizi tunazitoa kwa serikali za vijiji ili izielekeze katika ujenzi wa miundombinu ya serikali pamoja na miradi mingine ya maendeleo,” amesema Mkuu wa Wilaya huyo.

Akizungumza na Pipa la Habari, Mwenyekiti wa Kijiji cha Magunhumwa, Salum Mohammed, amesema kuwa wananchi wake, ambao kimsingi ndio waathirika wa maafa yaliyotokea wamesikitishwa sana hatua hiyo kwakuwa waliamini kuwa serikali inaweza angalau kuwagawia vifaa hivyo vya ujenzi ili waanze ujenzi wao wenyewe kwa ajili ya makazi yao.

“Kwakweli wananchi wamepokea taarifa hii kwa masikitiko.  Lakini haina namna kwakuwa serikali ndiyo imeshasema.  Wananchi wamelalamika sana kwasababu tayari kuna nyumba tatu ambazo zilikuwa zimeshajengwa na Kampuni ya Madini ya ACACIA na nyumba mbili ambazo zilijengwa na serikali kama mfano na kugawiwa kwa wananchi.  Hivyo, wananchi waliosalia waliamini kabisa nyumba zingine zitajengwa, ikizingatiwa vifaa vya ujenzi kama saruji na mabati vilikuwa vimekwishakutolewa na wahisani mbalimbali,” amesema.

Machi 12, 2015, Rais wa Tanzania, Dk. Jakaya Kikwete (wakati huo), alitembelea Mwakata na kuahidi kuwa serikali itahahakikisha makazi ya waathirika yanarejea katika hali ya kawaida kwa kuwajengea nyumba, ambapo aliahidi kuwa serikali itatoa shilingi bilioni 2 na aliagiza Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kujenga nyumba hizo bila kupitia mkandarasi yeyote kama ulivyo ujenzi wa serikali na kwakuwa ujenzi wa jeshi unaisha kwa wakati mfupi na hakuna uchakachuaji.
MISAADA YA WAATHRIKA WA MVUA MWAKATA KUJENGA MIUNDOMBINU YA SERIKALI MISAADA YA WAATHRIKA WA MVUA MWAKATA KUJENGA MIUNDOMBINU YA SERIKALI Reviewed by Unknown on 07:49 Rating: 5

No comments:

Theme images by merrymoonmary. Powered by Blogger.