ANGUKO SHULE ZA SERIKALI TUSITAFUTE MCHAWI KUTOKA NJE, NI SISI WENYEWE

Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi. Prof. Joyce Ndalichako.
Na Dotto Bulendu
Wakati huo shule za serikali kama shule za sekondari Azania, Mwanza, Mwenge, Mzumbe, Ilboru, Kilakala, Loreza, Mazengo, shule ya wavulana Tabora, Milambo, Rugambwa,Ihungo, Tosamaganga, shule ya ufundi Tanga (Tanga Tech), Msalato, Jangwani, Mkwawa, zikifanya vizuri hatukuwa tunachimba madini, tulikuwa tunalima pamba, chai, mkonge,tumbaku, lakini pia tulikuwa tunafuga tu mifugo.
 Kipindi hicho uwekezaji ulikuwa mkubwa, shule za msingi za serikali zilikuwa wanafunzi wanagaiwa madaftari, wanakunywa uji bure, penseli na biki zilikuwa zinagaiwa.
 Waliofaulu kwenda sekondari walikuwa wanasafiri bure, chakula bure, shuleni ilikuwa ni sehemu salama, ukikosa kuchaguliwa shule za serikali ilikuwa ni kilio, unaweza kujifungia ndani wiki nzima ukilia kukosa nafasi ya kwenda shule ya serikali.
 Chuo Kikuu ilikuwa ni sehemu ya heshima, unakwenda Chuo Kikuu kwa gharama ze serikali, si mkopo kama ilivyo sasa.
 Vikaibuka vitoto fulani, vikaja na mawazo yao ya utaratibu mpya wa kuendesha uchumi wa dunia, vikauita SAPs, vikauza mawazo yao Benki ya Dunia (WB) na Shirika la Fedha Ulimwenguni (IMF), wakaletewa Waafrika wakiwemo watanzania.
 Vikasema hivi vitoto vya Chuo Kikuu kutoka Ulaya, eti mfumo huu wa elimu ni mbovu,serikali ijitoe kabisa, iache kubeba gharama za kuendesha elimu,vikasema si sawa serikali kugharamia elimu.
 Wakubwa wetu kama walivyo, yaani wao ni kama madodoki, hawawezi kukataa wala kuhoji, jambo likitoka Ulaya ama Marekani au Asia ni zuri hilo, wakamuona Mwalimu Nyerere kapitwa na wakati, wakakumbatia utandawazi na mawazo ya tuvijana tulivyobuni mradi wa SAPs, wakaanza sema ooooh, sasa shule watu wachangie.
 Mara ooh, kazi ya serikali siyo kuwahudumia watu wake, serikali zetu zikaanza kujiondosha kugharamia elimu yetu, viongozi wetu wakaanza kujenga shule zao binafsi na kuachana na shule wanazozisimamia.
 Enzi hizo za Julius Nyerere, Idara ya ukaguzi ilikuwa imara sana, si kila mtu alikuwa mwalimu, ilikuwa huwezi kwenda darasa la tano bila mtihani wa darasa la nne,ilikuwa huwezi kwenda kidato cha tano bila kufaulu kidato cha nne, ilikuwa huwezi kwenda kidato cha tatu bila kufaulu mtihani wa taifa wa kidato cha pili, huendi Chuo Kikuu bila ‘Principle pass’ mbili na ‘subsidiary’ moja zenye wastani wa 4.5.
 Haya yote yalifutwa, ikawa zigizaga, tukaanza kujenga shule bila nyumba za walimu, tukaanza kuajiri wahitimu wa kidato cha sita wasio na mafunzo ya ualimu eti tukaita Voda fasta, serikali ikajitoa kuendesha na kusimamia shule zake.
 Shule zikajengwa huku hazina hata kagari kadogo, enzi hizo karibu shule zote za serikali zilikuwa na magari makubwa, leo shule hazina hata pikipiki, walimu wanalalamika kila siku,hawana morali, wanafundisha wakiwa na mawazo (Go slow strike).
 Sasa serikalini kila mtu anachaguliwa, hakuna tena ushindani wa kuingia shule za serikali, ushindani umehamia shule binafsi, shule za Serikali leo hakuna mitihani ya kuchuja, kuna kipindi eti wastani wa kwenda kidato cha tatu kutoka cha pili ulishushwa mpaka asilimia 14 kutoka asilimia 21, wakati huko shule binafsi na seminari,ili utoke hatua moja lazima upate wastani wa asilimia si chini ya 50, wengine lazima upate asimilia 60, halafu tunataka shule za binafsi zifanye vizuri.
 Hatutakiwi kusaka mchawi kutoka nje katika hili la kufanya vibaya kwa shule za serikali, wachawi ni sisi wenyewe, tukubali kuwa tulikosea na tulifanya mambo ya ajabu ambayo leo yanatugharimu.
ANGUKO SHULE ZA SERIKALI TUSITAFUTE MCHAWI KUTOKA NJE, NI SISI WENYEWE ANGUKO SHULE ZA SERIKALI TUSITAFUTE MCHAWI KUTOKA NJE, NI SISI WENYEWE Reviewed by Unknown on 12:09 Rating: 5

No comments:

Theme images by merrymoonmary. Powered by Blogger.