TUNDU LISSU AMSHUKIA DK. MWAKYEMBE KUFUTA CHAMA CHA WANASHERIA TANZANIA

Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Harrison Mwakyembe.

Na Tundu Lissu

Mawakili wenzangu. Mimi binafsi sijashangazwa na kauli ya Dk. Mwakyembe, kwamba atakifuta Chama cha wanasheria Tanzania (TLS) kama kitajiingiza katika harakati za kisiasa.

Hii sio mara ya kwanza kwa viongozi wa serikali ya Tanzania kutoa vitisho vya kuifuta TLS.  Waziri Mkuu zamani hayati Edward Sokoine aliwahi kutishia hivyo katika kilele cha vita dhidi ya wahujumu uchumi mwanzoni mwa miaka ya 1980. 

Hata kabla ya hapo katika miaka ya 1960 na 1970 watangulizi wa Sokoine walijaribu kufanya hivyo hivyo.  Sababu ya kuanzishwa kwa Shirika la Sheria Tanzania (Tanzania Legal Corporation) kipindi hicho kulichagizwa na jitihada za kuondoa mawakili wa kujitegemea au mawakili wasiokuwa wa serikali.

Vitisho dhidi ya TLS vilirudi miaka ya 1990 wakati wa Augustino Lyatonga Mrema.  Kitu kimoja kiko common katika vitisho hivyo vyote.  Vitisho hivi vimetolewa kila wakati kwa TLS na mawakili wa kujitegemea wanapotumia uhuru wao kutetea utawala wa sheria na kupinga uvunjifu wa sheria katika nchi na matumizi mabaya ya madaraka miongoni mwa watawala.

Mawakili wakiwa kimya na TLS ikiwa mfukoni mwa serikali na wasipohoji matumizi mabaya ya madaraka basi wanakuwa ni watu wanaojipendekeza kwa serikali.

Kuna kitu kingine ambacho siku zote huwa kinatokea kwamba vitisho hivi havijawahi kufanikiwa na havitafanikiwa.  Rais wa kwanza wa Zanzibar, Sheikh Abeid Amani Karume alipiga marufuku uwepo wa taasisi binafsi za kisheria mara baada ya Mapinduzi ya Zanzibar ya 1964.  Tanzania ya leo sio Zanzibar ya miaka ya 1960 na 1970, hatutakubali udikteta wa aina ya Karume au wa aina nyingine yoyote kwenye Tanzania ya leo.

Inaelekea Dk. Mwakyembe hafahamu au anajisahaulisha jinsi ambavyo TLS na mawakili binafsi walivyo ambatanishwa kwenye mfumo wetu wa kikatiba na kisheria.  Kwa lugha nyepesi, ukifuta TLS maana yake ni kwamba hakuna wakili binafsi hata mmoja nchi nzima. 

Mfumo mzima wa kimahakama unategemea uwepo wa mawakili na kwa hiyo uwepo wa TLS.  Mahakama karibu zote zitashindwa kufanya kazi kusipokuwa na mawakili binafsi.  Vivyo hivyo itakuwa katika taasisi zingine za kisheria na kimahakama.

Aidha, kuna taasisi nyingi zilizoundwa na Katiba yetu - kama vile Tume ya Huduma za Mahakama (Judicial Service Commission) na Tume ya Mabadiliko ya Sheria (Law Reform Commission), ambazo zinakuwa zinaundwa kukiwa na uwakilishi wa TLS.

Kuna taasisi nyingine nyingi ambazo zimeanzishwa na sheria za kawaida ambazo uundwaji wake unakamilika kukiwa na uwakilishi wa TLS. Hilo agizo la kisheria, kikatiba na kisiasa litakalofanya kufutwa kwa TLS, ni kitu ambacho hakijawahi kutokea na wala haifikiliwi kuwa kitatokea kwa mtu mwenye akili timamu.

Dk. Mwakyembe ana akili timamu.  Anaweza kuwa anatania.  Hawezi kufuta TLS.  Anachotaka kufanya ni kuwatisha mawakili ili wachague watu wale wale wa miaka yote kuongoza TLS.  Anatutisha ili tuendelee na sura ile ile katika uongozi wa TLS.

Hataki tufanye mabadiliko yanayohitajika ili TLS yetu isichukue nafasi yake stahiki katika kuamua mustakbali wa nchi yetu na wa taaluma yetu.  Nawataka viongozi na wanachama wa TLS wamkemee Dk. Mwakyembe kwa nguvu kubwa zaidi.

Nawataka wagombea wenzangu wa nafasi mbali mbali za uongozi katika TLS wajitokeze hadharani na kulaani kauli ya Dk. Mwakyembe bila kujali tofauti. Wakinyamaza tutawajua wako upande wa nani? Sura ile ile ya uongozi wa TLS au mabadiliko. Na nitawaomba nyote mpige kura kulingana na hali hiyo. 
TUNDU LISSU AMSHUKIA DK. MWAKYEMBE KUFUTA CHAMA CHA WANASHERIA TANZANIA TUNDU LISSU AMSHUKIA DK. MWAKYEMBE KUFUTA CHAMA CHA WANASHERIA TANZANIA Reviewed by Unknown on 09:44 Rating: 5

No comments:

Theme images by merrymoonmary. Powered by Blogger.