MAKAMU WA RAIS ATAJWA DAWA ZA KULEVYA

Rais wa Venezuela, Nicholas Maduro (kulia) akiwa na Makamu wake, Tareck El Aissami. (Picha na AFP)
Venezuela
Marekani imetangaza vikwazo dhidi ya Makamu wa Rais wa Venezuela, Tareck El Aissami, kwa tuhuma za kuhusika na ulanguzi wa kimataifa wa mihadarati.  El Aissami ameongezwa kwenye orodha ya walanguzi wakuu wanaosakwa na Marekani.
Aidha tajiri maarufu wa Venezuela, Samark Lopez, amewekewa vikwazo kwa kutuhumiwa kama mshirika mkuu wa El Aissami.  Tareck El Aissami, aliteuliwa kama Makamu wa Rais na Rais Nicolas Maduro mwezi uliopita.
El Aissami amekanusha madai ya kuhusika na visa vyovyote ya jinai.  Lakini Lopez hajajibu hatua hizi za Marekani.  Vikwazo hivi vinamaanisha kwamba mali yote ya Makamu wa Rais iliyoko Marekani inashikiliwa huku akizuiwa kuingia nchini humo.
Wizara ya Fedha ya Marekani imesema kwamba, El Aissami alisimamia kuvukishwa kwa tani nyingi za mihadarati ndani ya Marekani kwa kutumia ndege au meli.
Kadhalika imeongeza kuwa alikua kwenye orodha ya waliopokea mulungula kutoka kwa mlanguzi mkuu wa mihadarati wa Venezuela aliyeko korokoroni, Walid Makled, ili kumkinga wakati akiendelea na biashara haramu.
El Aissami aliwahi kuwa Gavana wa jimbo la Aragua na pia akawa waziri wa Mambo ya Ndani na Sheria nchini Venezuela kati ya mwaka 2008 na 2012.  Taarifa zilizonadiwa na mashirika ya habari ya nchini Marekani, zinasema kuwa El Aissami alikua akichunguzwa na Marekani kwa kushirikiana na kundi la wapiganaji la Hezbollah nchini Lebanon.
Wakati akiwa Waziri wa Mambo ya Ndani, imedaiwa kuwa hati kadhaa za kusafiria za Venezuela zilipatikana zikitumiwa na wapiganaji wa Hezbollah.  Mapema mwezi huu wabunge 34 wa Baraza la Congress Marekani walimuandikia waraka Rais Donald Trump, wakimtaka kuweka vikwazo kwa baadhi ya Maofisa wa serikali ya Venezuela.
Walimtaja hasa Tereck Al Aissami, wakisema ana nafasi kubwa ya kuongoza nchi kama Makamu wa Rais na alistahili kuchukuliwa hatua kutokana na tuhuma zake kuhusika na ulanguzi wa mihadarati pamoja na kuwa mshirika wa kundi ambalo Marekani imeliorodhesha kama la kundi la kigaidi.
CHANZO: BBC 
MAKAMU WA RAIS ATAJWA DAWA ZA KULEVYA MAKAMU WA RAIS ATAJWA DAWA ZA KULEVYA Reviewed by Unknown on 10:22 Rating: 5

No comments:

Theme images by merrymoonmary. Powered by Blogger.