WATOTO NJITI 210,000 WANAZALIWA NCHINI HUKU 13,900 WAKIPOTEZA MAISHA KILA MWAKA

Mama akiwa amembeba mtoto njiti kwa njia ya kangaroo ili kumpatia joto.

Na Mtapa Wilson

Taasisi inayosaidia watoto wanaozaliwa kabla ya wakati maarufu kama ‘watoto njiti’ ya Doris Mollel Foundation imewaomba wadau mbalimbali wa afya nchini kujitolea kwa hali na mali katika jitihada zake za kuwasaidia watoto njiti wanaozaliwa nchini.

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Doris Mollel Foundation, Doris Mollel, amesema kuwa ripoti ya Shirika linalojishughulisha na afya ya mama na mtoto la Mamaye Afrika, mwaka 2014, inaonyesha kuwa kila mwaka watoto wanaozaliwa kabla ya wakati nchini ni 210,000, huku wanaopoteza maisha ni 13,900, kutokana na sababu zinazoweza kuepukika kama vile ukosefu wa vifaa tiba.

Doris amesema pia kwa mujibu wa takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) zinaonyesha kuwa takribani watoto milioni 15 wanazaliwa kabla ya wakati, hali inayosababisha kuongezeka kwa vifo vya watoto kwa asilimia 40 duniani kote.

Aidha Doris ameongeza kuwa kutokana na changamoto ya watoto njiti, taasisi yake imekuwa ikishirikiana na serikali kwa kusaidia watoto wanaozaliwa kabla ya wakati katika maeneo mbalimbali nchini.

“Mwaka 2015 tulisaidia watoto wapatao 4,015 katika hospitali 17 zilizoko katika mikoa mbalimbali 19 iliyopo nchini kwa kutoa vifaa tiba.  Mbali na vifaa tiba tunavyotoa kupitia wadau wetu wa Afya,” amesema.

Akielezea changamoto iliyopo, Doris amesema wananchi walio wengi bado hawana ufahamu juu ya tatizo zima la watoto wanaozaliwa kabla ya wakati, hivyo taasisi yake imekuwa na jukumu kubwa la kuwafikia wananchi walio wengi katika maeneo ya vijijini ili kuwapatia elimu ya kukabiliana na tatizo hilo.  Lakini changamoto kubwa imekuwa ni uhaba wa fedha, ambao unasababisha kushindwa kutoa msaada kwa watoto njiti wanaozaliwa.

“Sisi kama taasisi tumeamua kuhakikisha wananchi wanaelimika juu ya watoto wanaozaliwa kabla ya wakati na kutoa msaada wa vifaa tiba kwa watoto hao.  Ajenda ya Umoja wa Kimataifa ni kupunguza vifo vya watoto wanaozaliwa kabla ya wakati kwa asilimia 50 ifikapo 2025.  Hii ni changamoto kwetu na changamoto kubwa zaidi ni watu wengi hawana uelewa kabisa juu ya tatizo hili.  Wanawake walio wengi bado wanajifungulia nyumbani.”

“Lakini inawezekana tatizo likawa kubwa zaidi kwani bado wengi hawafiki hospitali.  Kwakweli ili tuwafikie tunahitaji uwekezaji mkubwa wa fedha.  Hivyo tunawaomba wadau mbalimbali ikiwemo kampuni, asasi za kiraia pamoja serikali kuunga mkono juhudi zetu za kukabiliana na tatizo hili ili kupunguza kama siyo kumaliza kabisa tatizo hili ifikapo 2025,” ameeleza Doris.  
WATOTO NJITI 210,000 WANAZALIWA NCHINI HUKU 13,900 WAKIPOTEZA MAISHA KILA MWAKA WATOTO NJITI 210,000 WANAZALIWA NCHINI HUKU 13,900 WAKIPOTEZA MAISHA KILA MWAKA Reviewed by Unknown on 10:38 Rating: 5

No comments:

Theme images by merrymoonmary. Powered by Blogger.