'FEZA BOYS' YATOA MSHINDI TUZO DSTV EUTELSAT AFRIKA

Kutoka kulia ni Mkurugenzi wa shule za Feza Tanzania, Ibrahim Yunus Rashid na Meneja Masoko wa Multichoice Tanzania, Alpha Mria akimkabidhi barua ya uthibitisho mshindi wa pili wa shindano la DSTV Eutelsat Afrika, Davids Bwana, ambaye ni mwanafunzi wa shule ya wavulana Feza, mbele ya Mama yake mzazi, Dk. Mbutolwe Esther Mwakitalu.  

Na Mtapa Wilson

Davids Bwana, ambaye ni mwanafunzi wa shule ya wavulana Feza nchini Tanzania amekuwa mshindi wa pili barani Afrika katika shindano la kuwania tuzo ya nyota wa DSTV Eutelsat, ambalo lilifanyika nchini Nigeria na washindi wake kutangazwa Februari 7, mwaka huu.

Tuzo ya nyota wa DSTV Eutelsat hushirikisha zaidi wanafunzi wa ngazi ya elimu ya sekondari, ambapo hutakiwa kuwasilisha kazi zao kwa njia ya kuandika insha au kuandaa bango kuhusu elimu ya anga hususani satelaiti kwa lengo la kukuza vipaji vya kiakili kwa wanafunzi ili kuleta mageuzi endelevu na yenye tija katika ulimwengu wa sayansi na teknolojia.

Tuzo ya nyota wa DSTV Eutelsat huandaliwa na kampuni ya Multichoice Afrika kwa kushirikiana na Shirika la anga la Eutelsat la nchini Ufaransa.

Ni mara ya sita kufanyika kwa tuzo hii barani Afrika na mwaka huu imeshirikisha shule takribani 1,000 na nchi 20 barani Afrika, ambapo mwanafunzi kutoka nchini Ethiopia, Leoul Mesfin, aliongoza katika uandishi wa insha juu ya elimu ya satelaiti akifuatiwa na mtanzania, Davids Bwana, jambo lililofanya kuwa mtu wa kwanza kushika nafasi ya juu zaidi katika shindano hilo kutoka ukanda wa Afrika Mashariki.

Wakati katika upande wa kuandaa bango juu ya masuala ya satelaiti, nafasi ya kwanza ilichukuliwa na mwanafunzi kutoka nchini Nigeria, Emmanuel Ochenje, kisha nafasi ya pili kuchukuliwa na mwanafunzi kutoka nchini Botswana, Aobakwe Letamo.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam, Bwana amesema kuwa amepata nafasi hiyo kutokana na jitihada kubwa alizoziweka pamoja na walimu wake katika kuandaa insha yake.

Amesema ilikuwa ni changamoto kubwa kwake kushiriki shindano hilo ambalo lilikuwa linahitaji kila mshiriki abuni satelaiti yake mwenyewe na kuielezea jinsi itakavyofanya kazi na kusaidia kuboresha hali ya kiuchumi na kijamii, jambo ambalo litasaidia kuharakisha maendeleo barani Afrika.

“kwa kifupi mimi binafsi, familia yangu na wazazi wangu, na pia wanafunzi wenzangu wote kwa ujumla tumefurahishwa sana na ushindi huu.  Bila shaka itakuwa changamoto kwa wanafunzi wenzangu kote nchini kushiriki kwa wingi katika tuzo hizi mwakani ili ikiwezekana tufanye vizuri zaidi na kuchukua nafasi zote za juu,” amesema.

Aidha Mkuu wa Kitengo ya Uhusiano wa Umma wa kampuni ya Multichoice Tanzania, Johnson Mshana, amesema kuwa nafasi aliyoipata Bwana katika shindano hilo ni uthibitisho tosha kuwa watanzania wana uwezo mkubwa wa kushindana katika anga za kimataifa.

“kitendo cha kijana huyu kuibuka miongoni mwa washindi katika shindano linaloshirikisha kazi bora kabisa kutoka mataifa 20 kote Afrika ni heshima kubwa sana kwetu.  Hii itawatia sana moyo wanafunzi wa Tanzania na hivyo kuongeza jitihada.  Bila shaka kabisa mwakani washindi wa kwanza pande zote watatoka Tanzania,” amesema.

Mkurugenzi wa shule za Feza nchini, Ibrahim Yunus Rashid, amesema kuwa ushindi wa mwanafunzi wao umewapa furaha kubwa sana kwa pamoja walimu, wanafunzi na wafanyakazi wote kwa ujumla.

“Tumetiwa moyo sana na tunaamini wanafunzi wetu na wafanyakazi wetu watakuwa na ari zaidi katika kusoma na kufanya kazi ili kushiriki mashindano mbalimbali ya kitaifa na kimataifa na bila shaka shule yetu itaendelea kufanya kazi vizuri,” amesema.

Naye mama mzazi wa Davids Bwana, Dk. Mbutolwe Esther Mwakitalu, alipongeza sana jitihada binafsi za mwanaye, walimu na wanafunzi wenzie, ambapo pia alitoa wito kwa wazazi wenzake kuwa karibu na watoto wao na kuwasaidia kwa hali na mali katika ukuaji wao wa kitaaluma kwakuwa elimu ndio urithi mzuri kwao na kwa vizazi vyao vijavyo.

Kutokana na ushindi alioupata Bwana, sasa atapata fursa ya kwenda Afrika ya Kusini kutembelea Ofisi za Multichoice Afrika pamoja na Shirika la Anga la Afrika Kusini akiwa kama mgeni maalum wa Multichoice Afrika.
'FEZA BOYS' YATOA MSHINDI TUZO DSTV EUTELSAT AFRIKA 'FEZA BOYS' YATOA MSHINDI TUZO DSTV EUTELSAT AFRIKA Reviewed by Unknown on 20:42 Rating: 5

No comments:

Theme images by merrymoonmary. Powered by Blogger.