WAKILI KIBATALA AKOSOA KAULI YA DK. MWAKYEMBE

Mkurugenzi wa Sheria, Katiba na Haki za Binadamu Chadema, Peter Kibatala (kulia) akiwa na Mwanasheria Mkuu wa Chadema Tundu Lissu.

Na Peter Kibatala

Kauli ya Waziri Mwakyembe kwamba serikali haitasita kufuta Chama cha Wanasheria Tanzania (TLS) inajibiwa kwa hoja nyepesi sana; nini kimemstua?  Mbona hakuongea pale Jaji Mkuu Mstaafu, Augustino Ramadhani, alipochukua fomu za kugombea Urais kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM)?

Alihoji ni lini Jaji Augustino Ramadhani alichukua kadi ya uanachama ndani ya CCM?  Au kwa Waziri Mwakyembe ni sawa tu kwa Marais wa zamani TLS kugombea Ubunge kupitia CCM muda mfupi baada ya kuachia nafasi; na kutengeneza kila sababu kuwa walikuwa wanachama hai wa CCM wanaomiliki kadi?

Waziri Mwakyembe anafikiri Mawakili (taaluma ambayo yeye amejipumzisha nayo kwa muda na halipii ada ya uanachama wake kwa muda sasa kwa kuwa si taaluma anayoitumikia) hawana utashi wa kutosha kutofautisha kati ya itikadi za kisiasa na msingi wa TLS?  

Mawakili zaidi ya 5,000 wanaweza kuwa wajinga kiasi cha kurubuniwa na itikadi au harakati za kisiasa za vyama?

Alikuwa wapi yeye kama Wakili japokuwa ni taaluma yake, ambayo haitumikii, kutetea tulipotishiwa kuunganishwa katika kesi iwapo tutatetea wateja wetu?  Alikuwa wapi kukemea polisi walipokamata Mawakili wenzake wakiwa kazini?

Waziri Mwakyembe anafikiri ni rahisi kiasi hicho kuifuta TLS kwa kuwa yeye ni Waziri?  Hafahamu kuna Mahakama ambazo yeye hazisimamii na kuna taasisi zake kama vyombo huru vya kimahakama na vinginevyo?

Alikuwa wapi kuzungumzia Maafisa wa Polisi waliostaafu na punde tu wakagombea Ubunge kupitia CCM?  Tena hawa walikuwa Mawakili na wanachama wa TLS.  Mbona hakuzungumzia hali ya kutokupendelea ya Jeshi la Polisi?

Vipi kuhusu Mwanajeshi aliyeteuliwa nafasi ya juu CCM?

Watuache TLS tuchague viongozi wetu ili tuitimize majukumu yetu ya kisheria.
WAKILI KIBATALA AKOSOA KAULI YA DK. MWAKYEMBE WAKILI KIBATALA AKOSOA KAULI YA DK. MWAKYEMBE Reviewed by Unknown on 18:01 Rating: 5

No comments:

Theme images by merrymoonmary. Powered by Blogger.