VICTOIRE INGABIRE, KIONGOZI WA UPINZANI RWANDA NA MFUNGWA WA KISIASA MIAKA 15 GEREZANI

Kiongozi wa Upinzani na Mfungwa wa kisiasa nchini Rwanda, Victoire Ingabire.

Na Malisa Godlisten
Victoire Ingabire, kiongozi wa Chama cha Upinzani cha FDU nchini Rwanda, ni mfungwa wa kisiasa ambaye anatumikia kifungo cha miaka 15 jela kwa tuhuma za uhaini.
Victoire amekuwa mwanaharakati wa kutetea haki za binadamu na utawala bora kwa muda mrefu kabla ya kuamua kujiingiza rasmi kwenye siasa mwaka 2009.  Alizaliwa mwaka 1968 kupata elimu ya msingi na sekondari nchini Rwanda, kabla ya kwenda nchini Uholanzi kwa ajili ya elimu ya juu, ambapo alitunukiwa shahada ya kwanza ya Sheria za Biashara na Uhasibu (Commercial Law &Accounting) na Shahada ya pili ya Uchumi (Business Economics).
Baadae alifanya kazi katika taasisi kadhaa za kifedha nchini Uholanzi kabla ya kuamua kujiingiza kwenye siasa rasmi.  Victoire pia amewahi kushiriki katika harakati mbalimbali akiwa mwanafunzi na baadae mtumishi nchini Uholanzi.  Mwaka 1998 alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa RDR kwa wanyarwanda waishio nchi za Ulaya.
Mwaka 2010 aliacha kazi nchini Uholanzi na kurudi Rwanda na kujiingiza rasmi katika siasa.  Mwaka huohuo alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vikuu vya Upinzani nchini humo (RDR), na mgombea Urais kupitia vyama hivyo akitarajiwa kuchuana Rais Kagame.  Lakini jina lake liliondolewa na Tume ya uchaguzi nchini humo na akafungiwa kujihusisha na masuala ya kisiasa, kwa madai ya kufanya njama za kumpindua Kagame.
Siku chache baadae (October 14) mwaka huohuo alikamatwa na kushtakiwa kwa makosa ya uhaini ambapo upande wa Jamhuri uliiambia mahakama kuwa Victoire alishirikiana na baadhi ya wanajeshi katika jeshi la Rwanda na kula njama za kupindua serikali ili kumuondoa madarakani Rais Kagame.
Katika kesi hiyo Victoire alishtakiwa pamoja na viongozi kadhaa wa jeshi la Rwanda akiwemo Kanali Tharcisse Nditurende, Luteni Kanali Noel Habiyaremye, Luteni Jean Marie Vianney Karuta na Meja Vital Uwumuremyi.  Wote kwa pamoja walipatwa na hatia na kutupwa gerezani ambapo Victoire alihukumiwa kifungo cha miaka nane gerezani.
Lakini alikata rufaa ya kupinga adhabu hiyo kwenye mahakama ya juu (Supreme Court).  Rufaa ya Victoire ilikua na hoja mbili.  Hoja ya kwanza ni kwamba, makosa aliyodaiwa kuyatenda si ya kweli kwa sababu kipindi ambacho makosa hayo yanadaiwa kutendeka alikua uhamishoni nchini Uholanzi.  Kwahiyo asingeweza kupanga mbinu za kumpindua Kagame akiwa uhamishoni.
Pili Victoire alipinga hukumu hiyo akidai kuwa sheria ilitumika kinyume cha utaratibu.  Sheria iliyompata na hatia ilitungwa mwaka 2008 wakati anadaiwa kutenda kosa mwaka 2007. Wakili wa Victoire aliiambia mahakama kuwa si sahihi kutumia sheria kinyumenyume (the law should not be used retrospectively but retroactively).
Pia Luteni Kanali Michel Habimana aliyekua shahidi katika kesi hiyo aliiambia mahakama kuwa upande wa Jamhuri ulifanya upotoshaji na udanganyifu katika ushahidi.  Alisema ushahidi mwingi uliowasilishwa na Jamhuri ulikua umetengenezwa kwa lengo la kuwatia hatiani Victoire na wenzie.
Alisema maafisa wengi wa jeshi waliotoa ushahidi mahakamani walikuwa wameambiwa maneno ya kusema na walipachikwa vyeo bandia ili ushahidi wao uwe na nguvu.
Baada ya mahakama hiyo kusikiliza hoja za pande zote mbili ilisema kwamba, kifungo cha miaka nane gerezani aliyopewa Victoire ni kidogo kulinganisha na makosa aliyofanya.
Kwahiyo mahakama hiyo ilimuongezea adhabu ya miaka saba na kufanya kifungo chake kiwe miaka 15.  Luteni Kanali Habimana nae alihukumiwa kifungo japo inadaiwa kuwa baadae aliuawa kwa siri akiwa gerezani.
Victoire Ingabire ni mke na mama wa watoto watatu.  Anategemea kumaliza kifungo chake mwaka 2025.



VICTOIRE INGABIRE, KIONGOZI WA UPINZANI RWANDA NA MFUNGWA WA KISIASA MIAKA 15 GEREZANI VICTOIRE INGABIRE, KIONGOZI WA UPINZANI RWANDA NA MFUNGWA WA KISIASA MIAKA 15 GEREZANI Reviewed by Unknown on 16:42 Rating: 5

No comments:

Theme images by merrymoonmary. Powered by Blogger.